EDWARD Lowassa, Waziri Mkuu wa zamani, amemtaka Rais John Pombe Magufuli aendelee kufinya katika uongozi wake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Lowassa ametoa kauli hiyo leo Jumamosi tarehe 11 Julai 2020, katika Mkutano Mkuu wa CCM, unaofanyika jijini Dodoma.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania, ametoa kauli hiyo wakati anaelezea mafanikio yaliyofanywa na Rais Magufuli, katika uongozi wake.
Lowassa amesema, hakuna ubishi kwamba nchi imetulia na inaendelea vizuri na kwamba Rais Magufuli anatakiwa aongeze kasi katika utekelezaji wa sera zake.
“Hakuna ubishi yale mambo ambayo yalikuwa hayawezekani, yanawezekana chini ya uongozi wako. Hakuna ubishi kwamba nchi imetulia, inaendelea vizuri tunakuomba uendelee kufinya, kasi isipungue iendelee vilevile,” amesema Lowassa.
Lowassa alikuwa mpinzani mkali wa Rais Magufuli katika uchaguzi mkuu wa tarehe 25 Oktoba 2015 ambapo alikuwa mgombea urais wa Chadema akiungwa mkono na vyama vinne vya upinzani vya CUF, NCCR-Mageuzi, NLD na CUF.
Katika uchaguzi, Lowassa alitoa upinzani na kufanikiwa kupata kura milioni sita sawa na asilimia 39 huku Magufuli akipata kura milioni nane sawa na asilimia 58 ya kura zote zilizopigwa milioni 15.
Hata hivyo, Lowassa aliyejiunga na upinzani tarehe 28 Julai 2015 baada ya jina lake kukatwa ndani ya CCM katika mchakato wa kumpata mgombea urais na tarehe 1 Machi 2019, Lowassa alitangaza kurejea CCM.
Naye Cleopa Msuya, Waziri Mkuu Mstaafu amemuomba Rais Magufuli aendelee na kasi aliyoanza nayo tangu alipoingia madarakani tarehe 5 Novemba 2015.
Msuya amesema Rais Magufuli amefanikiwa kuitoa nchi katika umasikini na kuifikisha katika uchumi wa kati huku akiwataka wananchi kumchagua tena katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.
“Naungana na aliyosema rafiki yangu Lowassa, kwa sababu tumetoka kwenye umasikini na kuingia uchumi wa kati, kasi iendelee. Walio vijijini wachague watakaoungana nawe kusukuma gurudumu,” amesema Msuya.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online kwa habari zaidi
Victor chirambo 786docom