EDWARD Lowassa, Waziri Mkuu wa zamani nchini Tanzania, amemtumia ujumbe mgombea urais wan chi hiyo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Magufuli kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Monduli … (endelea).
Lowassa ametuma salamu hizo jana Jumatano tarehe 2 Septemba 2020, katika mkutano wa kampeni Uwanja wa Barafu uliopo Kata ya Mto wa Mbu alipokuwa akimnadi mwanae, Fredrick anayegombea Ubunge Monduli jijini Arusha.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini alimtuma, Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu akamwambie Rais Magufuli kwamba kuna zawadi yake ya kura kutoka kwa wananchi wa Monduli na Tanzania kwa ujumla.
“Majaliwa ukienda mwambie Rais Magufuli kuna zawadi moja tu ya kura kutoka kwa WanaMonduli,” alisema Lowassa.
Lowassa aliyekuwa Mgombea Urais wa Tanzania mwaka 2015 kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa mwamvuli wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) alisema, Magufuli anapaswa kupigiwa kura kutokana na kazi nzuri aliyofanya.
“Nimuombee kura Rais Magufuli, ametuongoza katika muda wa miaka mitano, amefanya maajabu sana. Nataka niseme moja tu, ni kiongozi wa ajabu hapa duniani. Tuongozaneni kupiga kura, mumchague pamoja na wagombea wa CCM,” amesema Lowassa.
Wakati huo huo, Lowassa amemuombea kura Fredrick, akiwataka WanaMonduli kumchagua siku ya kupiga kura.
Naye Waziri Majaliwa amemuombea kura Rais Magufuli pamoja na Fredrick.
“Leo niko mbele yenu kwa kazi moja tu, kuomba kura Watanzania wote na wanaMonduli, naomba kura za WanaCCM wote bila kujali vyama vyenu mumpigie kura Rais Magufuli na Fredrick Lowassa,” amesema Majaliwa.
Akizungumza katika mkutano huo, Fredrick ameomba kura akiahidi kushughulikia tatizo la migogoro ya ardhi.
“Migogoro ya ardhi ni jambo kubwa sana, kama tunavyofahamu ardhi haiongezeki bali sisi tunaongezeka, migogoro ikizidi inaleta chuki. Nitaenda kuitatua,” amesema Lowassa aliyewahi kuliongoza jimbo hilo kwa zaidi ya miaka 15.
Leave a comment