MGOMBEA Urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu amesema, mpinzani wake wa karibu Dk. John Magufuli, anayegombea nafasi hiyo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), hakujiandaa na kinyang’anyiro hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Singida … (endelea).
Lissu ametoa kauli hiyo leo Jumamosi tarehe 17 Oktoba 2020 katika mkutano wake wa kampeni alioufanya wilayani Manyoni mkoa wa Singida.
Katika Uchaguzi huo vyama 15 vimesimamisha wagombea wa Urais wa Tanzania, lakini Lissu na Dk. Magufuli wanatajwa kuwa na ushindani mkali kutokana na nguvu ya vyama vyao lakini pia ushawishi wao kwa wananchi.
Lissu amesema, Dk. Magufuli anayemaliza muda wake wa Urais wa Tanzania alifikiri Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020 utakuwa mwepesi kutokana na chama chake kufanya siasa peke yake katika kipindi cha miaka mitano tangu Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ulipomalizikia.
Mwanasiasa huyo amesema, Dk. Magufuli hakutegemea kukutana na ushindani mkali kutoka kwa vyama vya upinzani hasa Chadema, hivyo alijiandaa kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania.
“Dk. Magufuli hakuwa amejiandaa na uchaguzi huu, ndio maana mnaona hizi shida anazopata, alikuwa amejiandaa kutawazwa rais kama anavyotawazwa mfalme. Hawakuwa wametegemea uchaguzi wa aina hii kwa sababau kwa miaka mitano walijaribu kutumaliza Chadema,” amesema Lissu.
Lissu amesema, uchaguzi wa mwaka huu ni muhimu kuliko chaguzi zilizopita kwa kuwa wananchi wataamua muelekeo wa nchi katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Lissu amewaomba wananchi wa vyama vyote kuhamasishana kwenda kupiga kura.
“Zimebaki siku kumi tu, katika siku hizi kumi, hakikisheni mnahamasishana kila mmoja wenu, uwe CCM umepigwa, uwe Chadema umepigwa, uwe huna chama umepigwa. Sababu tumepigwa wote, tuhamasishane tarehe 28 Oktoba wote tukapige kura,” amesema Lissu.
Leave a comment