MWANASHERIA Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, amepeleka ombi katika Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, akiomba kumshtaki Job Ndugai, Spika wa Bunge na George Mkuchika, mwenyekiti wa Kamati ya Maadili, Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge, anaandika Dany Tibason.
Lissu anaomba kuwashtaki Ndugai na Mkuchika kwa kuwafungia kuhudhuria vikao vya Bunge wabunge watatu wa Chadema ambao ni Halima Mdee (Kawe), John Mnyika wa Kibamba na Ester Bulaya wa Bunda.
“Tumepeleka maombi ili Mahakama Kuu ili iweze kutoa amri ya kufutilia mbali uamuzi wa Spika wa Bunge letu wa kumsimamisha Mnyika kwa vikao saba vya bunge hili la saba.
Pia tunaiomba mahakama ifute uamuzi wa Bunge wa kuwasimamisha Mdee na Bulaya kuhudhuria vikao vilivyobaki vya Bunge hili na vikao vya Bunge la nane na Bunge la tisa,” amesema.
Amewaeleza wanahabari leo mjini Dodoma kuwa uamuzi wa Spika ulikuwa na upendeleo kwani uliwanyima haki wabunge wa upinzani kwa manufaa ya serikali na chama taewala.
“Tumeenda mahakamani ili pia tuweze kujua je mamlaka ya Bunge ya kumsimamisha Mbunge yana ukomo, je Bunge linaweza likaamua likamsimamisha Mbunge kwa vikao vyote ishirini?”
Katika mkutano huo na wanahabri, John Heche, John Heche alieleza kuwa jeshi la polisi linamuwinda ili kumkamata kwa tuhuma za uchochezi kufuatia hamasa aliyoitoa kwa wananchi wa jimbo lake kuwa wazuie wizi wa rasilimali unaoendelea.
“Nasema kwa kurudia tena, nipo tayari kukamatwa na nitatoka nje ya ukumbi wa Bunge, waje tu kunikamata, siogopi kitu wala mtu yoyote.
“Mimi nimetumwa na wananchi nije niwasemee hapa na narudia tena, kama Rais amesema watu wa Acacia ni wezibasi wananchi wa Tarime wana haki ya kuwakamata wezi hao katika maeneo yao,” amesisitiza.
Leave a comment