TUNDU Lissu, Mbunge wa Singida Mashariki ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Kisutu kuwa uchaguzi wa marudio wa Zanzibar haukuwa uchaguzi halali kisheria, anaandika Faki Sosi.
Lissu amedai hayo leo alipokuwa akijibu maelezo ya awali katika kesi ya uchochezi inayomkabili pamoja na Simon Mkina, Mhariri mkuu na mmiliki wa gazeti la MAWIO, Jabir Idrissa, mwandishi mwandamizi wa gazeti hilo Ismail Mahboob, mchapishaji kutoka kampuni ya Flint.
Katika kesi hiyo Na. 208 ya mwaka 2016 ambapo wanatuhumiwa kula njama na kutoa chapisho la uchochezi katika Gazeti la MAWIO, toleo Na. 182 la tarehe 14-20 Januari 2016.
Patrick Mwita wakili wa Serikali mbele ya Thomas Simba aliwasomea maelezo ya awali ya kesi inayowakabili.
Idrissa alikuwa mtuhumiwa wa kwanza kusomewa na maelezo hayo, alifuatiwa na Mkina pamoja na Mahboob huku Lissu akimalizia mwishoni.
Pamoja na kufanana kwa maelezo ya watuhumiwa hao lissu alikanusha wazi wazi kuwa kuwa uchaguzi wa Zanzibar hakuwa halili na kinyume na sheria.
Lissu amedai kuwa yeye sio mchapishaji magazeti kama ilivyoelezwa katika maelezo ya kesi hiyo na kwamba si kweli kuwa yeye angeweza kusababisha hofu kwa wananchi wa Zanzibar huku akisisitiza kuwa uchaguzi wa marudio Zanzibar, tarehe 20 Machi, 2016 haukuwa halali kisheria.
Mashtaka yanayowakabili
Shitakala la kwanza ni la kupanga njama za kutoa chapisho la uchochezi, kosa linalodaiwa kutendwa kati ya tarehe 12 na 14 Januari mwaka huu ambapo;
Idrisa, Mkina na Lissu katika eneo lisilojulikana jijini Dar es Salaam wanadaiwa kupanga njama za kuchapisha taarifa za uchochezi.
Shitaka pili linamkabili Jabir, Mkina na Lissu, wakidaiwa kuchapisha chapisho la uchochezi katika Gazeti la MAWIO, toleo Na. 182 la tarehe 14-20 Januari 2016.
Shitaka la tatu linamkabili Mahboob akidaiwa kuchapisha chapisho la uchochezi katika gazeti hilo lenye kichwa cha Habari ‘Machafuko yaja Z’bar’.
Shitaka la nne linamkabili Mahboob akidaiwa kuchapisha gazeti bila kupeleka kiapo kwa Msajili wa Magazeti, shitaka la tano linawakabili Idrissa, Mkina na Lissu wakidaiwa kuchochea hofu miongoni mwa wananchi kwa kuchapisha habari, “Machafuko yaja Zanzibar” na kwamba habari hiyo ingeweza kuzua vita au umwagaji damu.
Kesi hiyo itatajwa tena mfululizo tarehe 13 na 15 mwezi Februari ambapo upande wa Jamhuri utafika mahakamani hapo na mashahidi.
Leave a comment