TUNDU Lissu, mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ameahidi kukwapua ardhi iliyotwaliwa na vigogo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Ifakara..(endelea).
Mbele ya wananchi wa Ifakara, Morogoro tarehe 12 Agosti 2020, kwenye kampeni za kusaka urais amesema, serikali atakayoiunda itawashughulikia wezi wa ardhi.
“Kama wamechukua ardhi kwa kiwango hiki, watakubalije mpinzani aingie na kuibua ufisadi wao?” Amehoji Lissu.
Amesema, atafanya mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa umiliki ardhi kwa kuwa, vigogo wengi wamekwapua ardhi ya wananchi.
“Kuna vigogo wengi wamejimilikisha ardhi hapa, wakubwa hawa wametumia madaraka yao vibaya, wameiba ardhi ya wananchi na kuwafanya wahangaike.
“Maelfu ya heka yamekaa bure kwasababu wakubwa wameyachukua. Wananchi wanahangaika, hawana pa kulima,”amesema Lissu.
Amewaambia wakazi wa Ifakara, kwamba endapo atapata ridhaa ya kuongoza, atakwapua mashamba hayo kutoka kwa vigogo wanaoyamiliki.
Amesema, baada ya kukwapua ardhi hiyo, ataikabidhi kwa wananchi waitumie kwa kilimo na ufugaji.
Amesema, Morogoro ni sehemu muhimu kwa uchumi wa nchi kwa kuwa, zaidi ya asilimia 70 ya sukari nchini inatoka kwenye ardhi ya mkoa huo.
“Bonde la Kilombero mpaka Mikumi linaweza kulisha nchi kwa mwaka mzima.
“Kuna matunda, samaki na hakuna zao linaloweza kukataa kustawi kwenye ardhi ya Morogoro, lakini mkoa huu umefanywa kama shamba la bibi,” amesema
Leave a comment