Anaandika Tundu Lissu
Sheria ya Uendeshaji wa Bunge, 2008, inasema Bunge litagharamia matibabu ya mbunge ndani na nje ya nchi. Aidha, Bunge litaweka utaratibu wa kila mbunge kupatiwa bima ya afya.
Wabunge wote wana bima ya afya ya NHIF kwa ajili ya matibabu yao pamoja na familia zao. Tatizo, kwa hiyo, sio sheria bali ni siasa.
Wakati wa Bunge la Spika Makinda na, tunaambiwa, Spika Sitta, hakukuwa na ubaguzi katika suala la tiba ya wabunge.
Aidha, masuala hayo, na masuala mengine yanayohusu haki na maslahi ya wabunge, yalisimimamiwa na Bunge lenyewe kupitia Tume ya Utumishi wa Bunge na Ofisi ya Katibu wa Bunge.
Matatizo na malalamiko yalianza mara ya Rais John Magufuli kuingia madarakani na Spika Ndugai kuchaguliwa Spika.
Mara tukaanza kutangaziwa kwamba sasa safari zote za wabunge lazima zipate kibali cha Ikulu ya Magufuli. Haikupita muda tukaanza kusikia kwa sasa matibabu yote ya wabunge lazima sasa yapate idhini ya Ikulu ya Magufuli.
Waliojitokeza hadharani kulalamikia utaratibu huu kwamba haupo kwenye sheria yoyote, walibezwa kwa kukosa uzalendo au, mbaya zaidi, kwa kutaka kufanya ufisadi. Kwa kifupi, Spika Ndugai alikabidhi mamlaka kidogo ya Bunge yaliyopo kwenye Sheria kwa Rais Magufuli.
Sasa tunavuna matunda ya utaratibu huu mpya: Spika Ndugai na wapambe wake na wapendwa wa Jiwe wanatibiwa nje ya Tanzania na kupatiwa posho za kujikimu wanapokuwa nje ya nchi kama kawaida.
Kwa upande mwingine, akina mwenzangu na mie kama marehemu Kasuku Bilago au Tundu Lissu tunajihangaikia au tunahangaikiwa na Wasamaria Wema, kwa kuwa hatuwezi kupata idhini ya Jiwe ya kutibiwa ndani au nje ya nchi.
Marehemu Bilago amejihangaikia mwenyewe kujitibu Ntyuka Hospital. Iliposhindikana, wabunge wenzake wa upinzani wamemchangia gharama ya ndege ya kumpeleka mpaka Muhimbili.
Hakwenda Muhimbili kama mgonjwa wa Bunge, ameenda kama mgonjwa wa kujitegemea. Sasa amekufa Bunge ndio sasa limetwaa msiba wake na kuufanya wa Bunge.
Bilago hakufaa kufunikwa hata shuka moja ya hospitali iliyogharamiwa na Bunge akiwa mgonjwa. Sasa anastahili kufunikwa kwa bendera ya Bunge au ya Taifa kwa sababu ameshakufa na hana madhara yoyote tena!!!
Leave a comment