JESHI la Polisi Tanzania limemkamata Tundu Lissu, aliyekuwa mgombea urais wa nchi hiyo kupitia Chadema katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano ya 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Taarifa za kukamatwa kwa Lissu, zimetolewa leo jioni Jumatatu tarehe 2 Novemba 2020 na John Mnyika, Katibu Mkuu wa Chadema.
Katika ukurasa wake wa Twitter, Mnyika ameandika “Polisi wamemkamata Tundu Lissu muda huu (ilikuwa saa 12:40 jioni). Taarifa zaidi zitafuata.”
Kukamatwa kwa Lissu ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Bara ni mwendelezo wa viongozi wa upinzani hususani wa Chadema kukamatwa na polisi.
https://twitter.com/jjmnyika/status/1323288970021785600?s=21
Tayari Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, inawashikilia Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, aliyekuwa mgombea ubunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, aliyekuwa meya wa Ubungo, Boniface Jacob na aliyekuwa meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita.
Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Lazaro Mambosasa alisema, wanamshikilia Mbowe, Jacob na Lema wakituhumiwa kuhamasisha maandamano kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika 28 Oktoba 2020.
Vyama vya Chadema na ACT-Wazalendo vilitangaza maandamano ya amani nchini nzima yasiyo na kikomo wakitaka uitishwe uchaguzi upya wakisema huo uliofanyika Tanzania Bara na Zanzibar ulikithiri ukiukwaji.
Leave a comment