ALIYEKUWA mbunge wa Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Tundu Lissu, ameapa kutorejea nchini mwake, hadi hapo serikali ya Rais John Pombe Magufuli, itakapomhakikishia usalama wake. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza katika mahojiano yake na kituo televisheni cha Sauti ya Marekani (VOA), Lissu alisisitiza kuwa hawezi kurudi Tanzania kwa kuwa bado kuna tishio la kuangamiza maisha yake.
“Nimebadili msimamo wangu wa kurejea Tanzania mwishoni mwa mwaka huu. Hii ni kwa sababu, bado naamini kuwa mazingira ya kiusalama kwangu, bado sio mazuri. Kuna watu kule nchini, wanaendelea kutoa vitisho kuwa wataangamiza maisha yangu,” ameeleza Lissu.
Anasema, “kuna watu wanaandika hadi kwenye mitandao ya kijamii. Kwamba ngoja aje, mara hii hatutakosea shabaha. Lakini serikali yangu imeshindwa kuchukua hatua.”
Lissu ambaye kwa sasa “anaishi uhamishoni” nchini Ubelgiji, tangu aliposhambuliwa kwa risasi nyumbani kwake, ‘Area D’ mjini Dodoma, amesisitiza kuwa hatarejea nchini, “hadi Magufuli na serikali yake, wanihakikishie usalama wa maisha yangu.”
Shambulio dhidi ya Lissu lilitokea mchama wa tarehe 7 Septemba 2019, wakati mwanasiasa huyo machachari nchini alipokuwa akirejea nyumbani kwake, kutokea ofisi za Bunge.
Lissu alikuwa ameshiriki mkutano wa Bunge wa asubuhi; mara baada ya kushambuliwa alikimbizwa kwenye hospitali ya mkoa wa Dodoma na baadaye Nairobi nchini Kenya. Alifikishwa Ubelgiji, Januari mwaka 2018.
Akiongea kwa hisia kali, Lissu ambaye alipigwa risasi kadhaa mwilini mwake alisema, “…kuna mtu anaitwa Musiba. Ametangaza mitandaoni na kusema hadharani, kwamba Lissu atapigwa risasi siku akitua tu nchini.”
Akijibu swali la kipi kimemsukuma kubadilisha maamuzi yake ya kurejea nyumbani mapema na kama ambavyo alitangaza, Lissu anasema kwa njia ya kuhoji, “katika mazingira ambayo watu wantangaza hadharani kukuangamiza na huku serikali ikinyamazia kauli hizo, unawezaje kurudi nchini bila kuhakikishiwa usalama wako?”
Anasema, ni kweli kuwa amekamilisha matibabu yake nchini Ubelgiji na anajiona yuko imara na kwa hiyo, hana sababu ya kiafya ya kuendelea kukaa huko tena. Ninachotaka sasa, viongozi wenzangu walioko Tanzania waniambie kwamba mazingira yako sawa, ya kiusalama ya mimi kurudi.”
Lissu amesema, hadi sasa watu waliompiga risasi hawajachukuliwa hatua, na kwa hivyo, anahofia akirudi huenda wakamdhuru tena.
Lissu alitangaza angerejea nchini tarehe 7 Novemba mwaka huu; ndani ya chama chake, kulikuwa kumeanza kuandaliwa mipango ya mapokezi yake.
Hata hivyo, mwanasiasa huyo alishindwa kurejea na hakuna taarifa zozote ambazo zilitolewa kueleza kilichosababisha kushindwa kufanya hivyo.
Wachambuzi wa masuala ya kisiasa nchini wanasema, hatua ya Lissu kudai hakikisho la usalama wake, linaiweka serikali ya Tanzania katika wakati mgumu mno kwa kuwa kuendelea kukaa kwake nje, kunaichafua serikali hiyo na viongozi wake.
“Kama kuna mtu amemshauri Lissu kuchukua mkondo huu kabla ya kurejea nyumbani, basi huyo atakuwa amemsaidia sana. Maana sasa serikali italazimika kutoa hakikisho juu ya uhai wa mwanasiasa huyo, vinginevyo itaendelea kujichafua kwenye sura ya ulimwengu,” ameeleza kiongozi mwanasiasa mmoja ambaye alipata kuwa afisa wa juu kwenye Idara ya Usalama wa taifa (TIS).
Leave a comment