WAZIRI wa Afya, Ummy Mwalimu, amesema sekta zote zitaongeza nguvu, rasilimali fedha na rasilimali watu ili kuboresha kiwango cha lishe kwa Watoto wenye umri chini ya miaka mitano, wanawake wajawazito pamoja na vijana. Anaripoti Apaikunda Mosha TUDARCo … (endelea).
Haya ameyazungumza leo Ijumaa tarehe 30, Septemba 2022, katika hafla ya utiaji saini mkataba wa usimamizi wa shughuli za lishe.
Waziri Ummy ameeleza kuwa lishe bora ni msingi wa afya na uchumi wa mtu mmoja mmoja, familia na taifa kiujumla kwahiyo ili nchi iwe ya kipato cha kati “lazima tubadilike tuwekeze kwenye maendeleo ya rasilimali watu.”
Ameendelea kusema kuwa lishe mbovu inaleta utapiamlo mwilini na kusababisha madhara ya kiafya na kiuchumi na kuathiri maendeleo ya mtu na jamii kwa ujumla.
“Utapiamlo wa kupungua na kuongezeka kwa virutubisho mwilini unasababisha magonjwa yasiyo ya kuambukiza, udumavu na ukosefu wa akili,” amesema Mwalimu.
Amethibitisha kupungua kwa idadi ya watu wenye utapiamlo kwa mwaka 2015/16 mpaka kufikia mwaka 2018/19 kwa watoto chini ya miaka mitano wenye ukondefu kutoka asilimia 4.5 hadi 3.5 ambayo ni takribani watoto laki sita, na upungufu wadamu kwa wanawake wajawazito ilikuwa asilimia 45 na imepungua hadi kufikia asilimia 29 huk udumavu ukipungua kutoka asilimia 34 hadi 32.
Waziri ameeleza kuwa wizara ya Afya inalenga kuandaa na kutoa sera, miongozo na mikakati ya Afya ikiwemo huduma za lishe pamoja na kupunguza udumavu kwa watoto kwa kutekeleza hafua za lishe zinazolenga siku 1000 za maisha ya mtoto ikiwemo utoaji wa matone ya madini ya chuma na acid ya folic kwa mama wajawazito takribani million 2.3 kwa mwaka, kutoa matone ya vitamin A na dawa za minyoo mara mbili kwa mwaka kwa Watoto wenye umri chini ya miaka mitano na kusimamia kuongeza kwa virutubisho vya madini na vitamini kwenye vyakula na kutoa matibabu kwa Watoto wenye utapiamlo.
Aidha, Waziri amewataka wakuu wa mikoa kuhakikisha wanachukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Ebola ili kuhakikisha nchi inaepukana na ugonjwa huo ambao kwa sasa upo katika nchi ya Uganda ambao mpaka jana saa 4 usiku iliripoti wagonjwa 50 na vifo 28.
Leave a comment