KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC), kimeonya juu ya uibukaji mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi ‘Albino’ na kuitaka Serikali kuongeza juhudi za kuwalinda. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Tahadhari hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 11 Aprili 2022, jijini Dar es Salaam na Mtafiti wa LHRC, Fundikira Wazambi, katika uzinduzi wa Ripoti ya Haki za Binadamu ya 2021.
Wazambi amesema ripoti yao imebaini ongezeko la asilimia 30 la mauaji yanayisababishwa na imani za kishirika, ikiwemo ya watu wenye ualbino, ambapo mkoani Tabora ililiripotiwa mauaji ya mtoto mmoja.
“Imeripotiwa tukio moja la mtoto mwenye ualbino kuuawa Wilaya ya Uyui, mkoani Tabora, tangu 2015 hatukusikia hayo matukio ilikuwa kimya. Nadhani tuzidi kuongeza juhudi za kulinda ndugu zetu,” amesema Wazambi.
Wazambi amesema “pia iliripotiwa tukio la kufukuliwa kaburi la mtu mwenye ualbino, kama wameshindwa kutafuta mtu hai, watafute viungo vya aliyefariki na kuzikwa.”
Katika hatua nyingine, Wazambi amesema ripoti hiyo imebaini bado kuna matukio ya mauaji yanayofanywa na watu wanaojichukulia sheria mkononi, ambapo kwa 2021 kulikuwa na wastani wa matukio 39 kwa mwezi, huku Tanzania Bara ikiwa na idadi kubwa ya matukio hayo.
“Mauaji kwa kujichukulia sheria mkononi kulikuwa na wastani wa matukio 39 kila mwezi, hutokea asilimia kubwa upande wa Bara. Kuna sababu wananchi wamezitaja kwa nini wanachukua sheria mkononi ikiwemo kuona mshtakiwa yuko mtaani na kukosa imani na Polisi,” amesema Wazambi.
Leave a comment