IKIWA leo tarehe 8 Machi 2018 Tanzania na dunia nzima inaadhimisha siku ya wanawake duniani, serikali imeendelea kusisitizwa kuboresha sera na sheria zinazohusu wanawake ili kuimarisha ustawi wao. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Wito huo umetolewa leo na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Anna Henga akiwa nchini Marekani.
Henga ameitaka serikali kuendelea kufanya maboresho baadhi ya vifungu vyenye mapungufu vinavyokandamiza haki za wanawake katika sheria mbalimbali ikiwemo sheria ya mirathi.
“Ni vizuri tukawa na sera na sheria nzuri dhidi ya wanawake, sheria hizo zitasaidia wanawake kuwa na ustawi. Sheria za mirathi na zinazohusu ukatili wa wanawake zifanyiwe marekebisho,” amesema Henga.
Aidha, Henga ameitaka jamii kubadilisha mtazamo na fikra hasi dhidi ya wanawake ikiwa pamoja na kuondoa mfumo dume, badala yake iheshimu na kutimiza haki za wanawake.
“Jamii tubadilishe mtazamo, na fikra kwa kuwa na mtazamo chanya kwa wanawake sababu wako wengi idadi yao ni zaidi ya asilimia 50. Hivyo tukibadilisha mtizamo juu yao tutaleta amani, maendelea na mafanikio kwa jamii,” amesema Henga.
Tarehe 8 Machi kila mwaka ni siku ambayo dunia huadhimisha siku ya wanawake, ambapo huitumia siku hiyo kuangalia changamoto na mafanikio ya wanawake katika nyanja mbalimbali ikiwemo kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Leave a comment