MATOKEO ya ripoti ya nusu mwaka wa 2018 ya haki za binadamu nchini iliyoandaliwa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) yamebainisha kwamba ukatili dhidi ya watoto hasa ukatili wa kingono yameongezeka kwa kasi katika kipindi cha mwezi Januari hadi Juni mwaka huu. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Akizungumza na wanahabari wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo uliyofanyika leo tarehe 31 Agosti 2018 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga amesema ukatili wa kingono dhidi ya watoto aina ya ubakaji na ulawiti kwa nusu mwaka wa 2018, umeongezeka mara tatu zaidi ya ilivyokuwa katika kipindi cha nusu mwaka wa 2017.
Akifafanua kuhusu takwimu za matukio ya ukatili huo, Henga ameeleza kuwa, kati ya matukio 6,376 ya ukiukwaji wa haki za watoto yaliyoripotiwa kwenye vituo vya polisi katika kipindi cha nusu mwaka wa 2018, matukio 2,365 yalikuwa ya ubakaji na 533 yalikuwa ya ulawiti.
“Pia kumeongezeka ukatili dhidi ya wanawake ikiwemo ukatili wa kingono na kimwili, mfano matukio yaliyotokea katika kipindi cha mwezi Januari hadi Juni idadi ya wanawake 1,218 wameripotiwa kubakwa sawa na wanawake 203 kila mwezi,” amesema.
Naye Mtafiti wa LHRC, Fundikira Wazambi akielezea kuhusu matokeo ya ripoti hiyo kwa upande wa ukatili dhidi ya wanawake na watoto, amesema katika kipindi cha nusu mwaka wa 2018, asilimia 66 ya watoto wa kike waliripotiwa kubakwa wakati asilimia 34 ya wanawake waliripotiwa kubakwa.
“Matukio ambayo yametokea yaliyokiuka haki za binadamu katika kipindi cha miezi sita ni hali ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto hasa ukatili wa kingono, ikiwemo ubakaji. Wanawake waliobakwa ni asilimia 34 na watoto wa kike waliobakwa ni asilimia 66, watoto wa kike haki zao zimekiukwa zaidi kupitia ukatili wa kingono dhidi yao,” amesema.
Ripoti hiyo ya nusu mwaka hulenga kuangazia hali ya haki za kiraia, kijamii, kisiasa na haki ya makundi maalumu inavyoendelea.
Leave a comment