GODBLESS Lema Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema) ameshushiwa kipigo kutoka kwa walinzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaandika Mwandishi Maalum Arusha … (endelea).
Tayari taarifa ya kipigo hicho ameifikisha katika Jeshi la Polisi ambapo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Kamanda Ramadhani Ng’azi amethibitisha kupokea taarifa ya Lema kupigwa na walinzi wa CCM.
Wakati Lema akishambuliwa, Ibrahim Ismail ambaye ni wakala wa Chadema Kata ya Kaloleni mkoani humo ameripotiwa kushambuliwa kwa kuchomwa visu.
Mwingine aliyeshambuliwa kwenye tukio hilo na taarifa yake kumfikia Kamanda Ng’azi ni pamoja na Boniface Kimario, Mgombea Udiwani Kata ya Kaloleni pia Iddi Mukuru, Mwenyekiti wa CCM Kata ya Kaloleni anayedaiwa kujeruhiwa kwa kuchomwa visu na wafuasi wa Chadema.
Chadema ni miongoni mwa vyama vinavyoshiriki uchaguzi mdogo unaofanyika leo Jumapili katika maeneo mbalimbali Tanzania Bara.
Kufuatia vurugu hizo, Kamanda Ng’azi amesema polisi imefungua jalada la uchunguzi pamoja na kuanzisha msako wa kuwabaini waliohusika na vurugu hizo.
Amesema majeruhi walipelekwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru ili kupatiwa matibabu.
Leave a comment