ALLY Mohamed Mtiga, mwenyekiti wa kamati ya mazingira mtaa wa Tambukareli Kata ya Azimio wilayani Temeke, Dar es Salaam, anashikiliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru ), kwa tuhuma za kupokea rushwa ya Sh. 200,000. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi tarehe 4 Juni 2020 na Donasian Kessy, Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Temeke imesema walibaini uhalifu huo, baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa mwananchi ya kwamba Mtiga alimuomba rushwa hiyo.
“Mnamo tarehe 19 Januari 2019 Ofisi ya Takukuru Mkoa wa Temeke ilipokea malalamiko yanayomhusu Mtiga anaomba rushwa Sh. 200,000, kutoka kwa mwananchi ili aweze kumsaidia kupata leseni ya makazi ya jengo lake,” amesema Kessy .
Kessy amesema, baada ya Takukuru kupokea taarifa hiyo, ilimuwekea mtego Mtiga, ambao ulimnasa baada ya kukubali kupokea rushwa hiyo kutoka kwa mwananchi, ambaye alimuahidi kumpatia leseni ya makazi ya jengo lake, huku akijifanya ni Afisa Ardhi.
“Uchunguzi wa Takukuru ulibaini mnamo tarehe 26 Januari 2019, Mtiga ambaye anayejifanya Afisa Ardhi, akiwa ofisini kwa mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Tambukareli, alipokea fedha hizo za mtego kiasi cha Sh. 200,000 ili aweze kumsaidia mwananchi mmoja kupata leseni ya makazi ya jengo lake,” amesema Kessy.
Kessy amesema, uchunguzi kuhusu sakata hilo umekamilika na kwamba Mtiga atafikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Temeke, ambako amefunguliwa mashtaka kwa kosa la kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu.
“Takukuru imemkamata kwa kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu kinyume cha Sheria. Uchunguzi wa tuhuma hii umekamilika na mtuhumiwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani leo Alhamisi tarehe 4 Juni 2020,” amesema Kessy.
Leave a comment