MSHAMBULIAJI matata wa Arsenal, Alexandre Lacazette amewaachia ujumbe mzito mashabiki wa timu hiyo ya Ligi Kuu England baada ya klabu hiyo kutangaza kuwa ataondoka kwenye uwanja wa Emirates mkataba wake utakapokamilika mwishoni mwa mwezi huu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kupitia kwenye mtandao wa Instagram, jana tarehe 3 Juni, 2022 Lacazette ambaye alijiunga na Arsenal Julai 2017, aliishukuru klabu hiyo na mashabiki wake akisema kuwa kwa kuichezea Arsenal, ndoto yake ilikuwa imetimia.
Mfaransa huyo vilevile alidokeza kuwa alikuwa katika mapenzi na klabu hiyo na kwamba atasalia shabiki wa the Gunners hata baada aya kuondoka Emirates.
“Miaka mitano iliyopita, ndoto yangu ilitimia baada ya kujiunga na Arsenal. Imekuwa fahari yangu kuvaa nembo hii, kuwa mmoja wa familia hii. Nilishinda makombe, nilikutana na watu wazuri na kuzama katika mapenzi na klabu hii. Kila la heri kwa klabu na mashabiki. Imekuwa ni fahari. Mwana-Arsenal daima. Asante Arsenal,” Lacazette aliandika.
Tofauti na ilivyokuwa kwa aliyekuwa mshambuliaji mwenza wake Pierre-Emerick Aubameyang, Kocha mkuu Mikel Arteta amemshukuru Lacazette kwa kujitoa kuitumikia klabu hiyo ambayo alijiunga nayo miaka mitano iliyopita kutoka Olympique Lyon ya Ufaransa ambayo ni klabu yake ya nyumbani.
“Laca alikuwa mchezaji mahiri sana kwetu. Amekuwa kiongozi wa kweli ndani na nje ya uwanja na kuwa kielelezo kwa wachezaji wetu wachanga. Kujitolea kwake limekuwa jambo la kupigiwa mfano. Tunamtakia yeye pamoja na familia yake ufanisi na furaha,” Arteta amenukuliwa.
Lacazette mwenye umri wa miaka 31 amekuwa mfungaji bora wa Arsenal kwa misimu miwili- msimu wa 2017/18 na ule wa 2020/21 na kufurahia ufanisi chini ya makocha watatu tofauti.
Laca alishinda kombe la FA mwaka 2020, Ngao ya Jamii mwaka 2017, kuchaguliwa mchezaji bora wa Arsenal msimu wa 2018/19 na ameifungia Arsenal mabao 71 katika mechi 206 ambazo ameichezea.
Kabla kuhamia Emirates, Laca alikuwa amechezea klabu moja pekee tangu utotoni, Lyon, na kuifungia mabao 100 katika miaka saba ambayo aliichezea kwenye Ligue 1.
Taarifa za uhamisho zinamhusisha na kurejea Lyon, klabu ambayo alijiunga nayo akiwa mtoto mwaka 1998 akiwa na miaka saba tu na kupanda ngazi hadi kikosi cha kwanza mwaka 2010 akiwa na umri wa miaka 20.
Leave a comment