Akizungumza wakati wa kuwasilisha Makadirio na Mapato ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2019/20 tarehe 13 Juni 2019, Dk. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango, alisema serikali imerejesha kodi hiyo.
Wakizungumza na MwanaHALISI Online, baadhi ya wananchi wameeleza kutoridhishwa na hatuahiyo ya serikali.
Speratus Nyarusi, Mfanyakazi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP Mtandao) amesema, kitendo cha kurudisha kodi hiyo ambao ndio msaada mkubwa, si jambo jema na kuwa, serikali imeongeza msalaba na mzigo mkubwa kwa wanawake.
“Ukiangalia hali ya uchumi wa sasa na kipato ni cha kawaida, tulitarajia serikali ingeendelea kuwafuta machozi na kuwabeba, ni jambo limeonekana kuwakera wanawake wengi.
“Wanawake kitakwimu ni wengi sana nchini, na serikali ilitakiwa ikae na waazalishaji na wafanyabiashara wa taulo hizo kwa ajili ya kuangalia namna ya kutafuta ufumbuzi, wapo wanafunzi, itakuwa changamoto,” amesema.
Neofita Francis, Mkazi wa Mabibo amesema, mzigo umerudi kwa wanawake hivyo serikali ikae chini na kuangalia upya suala la kumpunguzia mzigo mzazi anayesomesha watoto wakike ambao wanahitaji taulo hizo kwa wingi.
“Utakuta mzazi ana watoto watatu wa kike, na wapo kwenye hedhi siku mbalimbali na inabidi bajeti yao lazima iwepo, haijalishi ni wakati gani,” amesema.
Neema Mwinyi, Mwanaharakati Ngazi ya Jamii amesema, mwaka jana na juzi wamepiga kelele kuishinikiza serikali kuhusu punguzo la tozo lakini jitihada ziligonga mwamba.
“Kiukweli hawakiututendea haki kodi ni kubwa na kama unavyojua hali ni zetu za kitanzania 2,000 ya kununua taulo za kike ndio hela ya chakula cha familia na kuna wanafunzi ambao mpaka sasa ikifika huo muda tunawaona, mtoto anashindwa hata kunyanyuka kujibu swali, tulitegemea serikali ingetupa bei elekezi katika mashule ili kutusaidia walimu na wanafunzi wetu.
“Bajeti ni kubwa na ikitokea watoto watatu wameingia kwenye siku zao ndani ya wiki moja, basi ujue tunakuwa na hali ngumu sana na mnajua taulo hizi sio bidhaa za chakula kwetu sisi ni utu”, amesema.
Salma Mohamed, Mkazi wa Magomeni amesema, ongezeko hilo litaleta athari kubwa hasa vijijini ambako watu hawana uwezo wa kumudu bei hivyo, wanawake kwa ujumla wao wapaze sauti wasizoee kuridhika.
Robert Swiga, Mkazi wa Mbezi Malamba Mawili, amesema serikali ipunguze kodi hiyo kwasababu gharama zinapoongezeka ndio mzigo unaongezeka.
“Mimi nina watoto watatu, unaponiongezea gharama kwenye kuwamudu kwenye masuala ya taulo za kike wanapofika kwenye wakati wao inakuwa changamoto kubwa, kwangu kama mzazi kwasababu nitashindwa kumudu zile gharama hivyo atashindwa kuudhuria masomo vizuri,” amesema.
Leave a comment