LEO Jumanne tarehe 27 Oktoba 2020 kura za mapema kwa watumishi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) na watumishi wanaosimamia uchaguzi huo, zinaendelea kufanyika visiwani humo huku baadhi ya wafuasi wa upinzani wakishikiliwa na Jeshi la Polisi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Watu kadhaa wanashikiliwa na Jeshi la Polisi visiwani Zanzibar kwa tuhuma za kuwafanyia fujo Askari Polisi waliokuwa wanasambaza masanduku ya kura usiku wa jana Jumatatu tarehe 26 Oktoba 2020.
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 27 Oktoba 2020 na Insekta Jenerali wa Polisi Tanzania, Simon Sirro wakati anazungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa kesho.
“Jana usiku Zanzibar huko Pemba, kuna vijana wakati tunasambaza masunduku ya kura wameanza kufanya fujo wanatupa mawe, jambo la ajabu unapotupa mawe na matokeo yake hao wa baadhi ya vijana wamekamatwa, sheria ikichukua mkondo wake matokeo yake ndoto zao zinapita,” amesema IGP Sirro.
IGP Sirro amesema “hatutarajii kutokuwa na vifo tusingependa hayo, lakini nategemea kama una silaha unatumia mawe lolote linaweza tokea.”
Kwa upande wake, Juma Sadi Khamis, Kamanda wa Polisi Kaskazini Pemba, amesema takribani watu 34 wanashikiliwa na Polisi kwa tuhuma za kuwarushia mawe askari polisi waliokuwa wanasambaza masunduku ya kura na kuchoma moto barabarani.
Kuhusu uwepo wa vifo kutokana na adhabu hiyo, Kamanda Khamis amesema, hakuna mtu yeyote hadi sasa aliyeripoti taarifa za vifo au majeruhi katika Jeshi la Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba.
“Kwa ujumla, hakuna yoyote ambaye ameripoti polisi kuna watu wamepoteza maisha au wamepata majeraha makubwa. Kwa ujumla, Pemba hali ni shwari hakuna taarifa hapa polisi za vifo isipokuwa tunasikia juu juu haijatihibitishwa,” amesema Kamanda Khamis.
Hata hivyo, Kamanda Khamis amesema zoezi la kura ya mapema linalofanyika leo linaendelea vizuri na hakuna fujo yoyote.
Kwa upande wake, Katibu wa Kamati ya Itikadi, Uenezi na Mahusiano na Umma wa ACT-Wazalendo, Salim Biman amesema, kuna baadhi ya watu wameuawa Pemba huku Unguja watu kadhaa wakijeruhiwa.
Bimani amesema, kwa sasa ACT-Wazalendo inakusanya taarifa za watu walipoteza maisha na kujeruhiwa kishakitatoa taarifa kwa umma.
“Hali ya Zanzibar ni mabomu kwenda mbele, vifo na majeruhi unguja na vifo vimetokea Pemba na majeruhi Unguja wengi tunao, siwezi kusema kama wangapi, kwa sababau tunakusanya ripoti kamili ila wanaweza kufika 50 au zaidi hapo,” amesema Bimani.
Amesema baadhi ya wafuasi wao na viongozi wa chama hicho wamekamatwa na Jeshi la Polisi, huku Mgombea wake wa Urais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad akiendelea kushikiliw ana polisi.
Leave a comment