BAADHI ya wabunge wa viti maalum wasio na chama katika Bunge la Tanzania, Halima Mdee na wenzake 18 wameshindwa kuamua juu ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2022/23 ya Sh.41.48 trilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamejitokeza leo Ijumaa tarehe 24 Juni 2022 wakati wa shughuli ya kuipigia kura bajeti hiyo ya serikali ambapo wabunge wote walikuwa wakiitwa kwa jina.
Awali, Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson alitoa maelekezo ya upigaji kura akisema zitakuwa za aina tatu, “ukiitwa jina utasema ndio, hapana au sina uamuzi (sijaamua)” na si vinginevyo.
Dk. Tulia alisema baadhi ya wabunge hawamo bungeni, “lakini ofisi ina taarifa zao na si vizuri kueleza changamoto zao” lakini itoshe kusema tuna taarifa zao.
Baadhi yao kwenye kundi hilo la Mdee na wenzake walipoitwa walisema ‘sijaamua’ huku wengine wakiwa hawamo bungeni.
Mdee na wenzake 18 wapo bungeni licha ya kutokuwa na chama kinachowawakilisha. Walifukuzwa Chadema tarehe 27 Novemba 2022 wakituhumiwa kwa usaliti, kughushi nyaraka za chama kisha kujipeleka bungeni kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalum.
Mbali na Mdee, wengine waliofukuzwa Chadema, ni waliokuwa wajumbe wa Kamati Kuu (CC), Esther Matiko na Ester Bulaya; aliyekuwa makamu mwenyekiti wa Bawacha (Bara), Hawa Subira Mwaifunga na aliyekuwa katibu mkuu wa Bawacha, Grace Tendega.
Wengine, ni aliyekuwa Katibu mkuu wa Baraza la Vijana la chama hicho (BAVICHA), Nusrat Hanje; aliyekuwa Naibu katibu mkuu wa Bawacha (Bara), Jesca David Kishoa; Cecilia Pareso, Agnesta Lambart, ambaye alikuwa mwenezi wa Bawacha na Tunza Malapa, aliyekuwa mwenyekiti wa Chadema, mkoani Mtwara.
Katika orodha hiyo, wamo pia Asia Mohammed, aliyekuwa Naibu Katibu mkuu wa Bawacha (Zanzibar), Felister Njau, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Stella Flao, Anatropia Theonest, Salome Makamba na Conchesta Rwamlaza.
Mbali na kina Mdee pia baadhi ya wabunge wa upinzani kupitia ACT-Wazalendo wamepiga kura kama hiyo ya ‘sijaamua.”
Maombi hayo ya kina Mdee, yaliondolewa mahakakani hapo juzi Jumatano, tarehe 22 Juni 2022 na Jaji John Mgetta kutokana na kasoro zilizobainika katika jina la mujibu maombi wa kwanza ambaye ni Chadema.
Jaji Mgetta alisema, Mdee na wenzake walipaswa kufungua maombi hayo kwa kutaja jina sahihi la bodi hiyo kwa mujibu wa sheria ambapo walitakiwa kuandika “Registered Body of Trustees” badala ya Body of Trusties, waliyoandika.
Kwa uamuzi huo wa Mahakama na Katiba ya Tanzania, Mdee na wenzake 18 walioapishwa tarehe 24 Novemba mwaka 2020 kuwa wabunge wa viti maalum walipoteza sifa za kuwa wabunge wa Bunge kwani ili uwe mbunge lazima uwe na chama na wao kwa sasa hawana chama cha siasa.
Mama Spika,
Kama bunge Lina taarifa za wabunge wasiokuwepo, basi useme wamepiga kura ipi….UWAZI NI SIRI YA MAENDELEO!
Kama hawaruhusiwi kupiga kura wakiwa nje ya bunge, tunaomba utuambie kama akidi ilitimia na waliokuwepo bungeni wamepitisha kwa kura ngapi.
MWANDISHI, andika kwa kufuata sheria za kura za Bajeti bungeni…siyo kurudia rudia majina ya wale 19.
Bajeti ilipitaje?