RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amemrejesha tena Alphayo Kidata kuwa Kamishan Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kidata amerejeshwa kwenye nafasi hiyo, aliyoitumikia miaka takribani minne iliyipota, baada ya kuteuliwa na aliyekuwa Rais, Hayati John Pombe Magufuli, Desemba mwaka 2015.
Safari ya Kidata kwenye utumishi tangu mwaka 2015, imekuwa ya kupanda na kushuka na sasa Rais Samia, ameamua kumteua kurejea kwenye nafasi hiyo kwa mara nyingine.
Kidata ameteuliwa Jumapili ya tarehe 4 Aptili 2021 na Rais Samia, akichukua nafasi ya Dk. Edwin Mhende.
Tangu kuingia madarakani kwa Rais Samia tarehe 19 Machi 2021, ameendelea na panga pangua ya wateule mbalimbali.
Samia aliingia madarakani baada ya aliyekuwa Rais Hayati Magufuli, kufariki dunia tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam na mwili wake, kuzikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita.
MwanaHALISI Online, linaangazia safari ya Kidata kuanzia mwaka 2015 hadi sasa.
Desemba mwaka 2015, Kidata aliteuliwa na Hayati Magufuli kuwa Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA. Baadaye alikuwa Kamisha kamili.
Kabla ya uteuzi huo, Kidata alikuwa katibu mkuu wa wizara ya ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi.
Nafasi hiyo ya Kamisha wa Mkuu wa TRA, alihudumu hadi tarehe 23 Machi, 2017 ambapo Hayati Magufuli alimteua kuwa Katibu Mkuu, Ikulu.
Kidata alihudumu nafasi ya Katibu Mkuu, Ikulu hadi tarehe 10 Januari 2018, alipoteuliwa na Hayati Magufuli kuwa Balozi wa Tanzania nchini Canada.
Safari ya Kidata kwenye utumishi iliingia doa tarehe 8 Novemba 2018, ambapo Hayati Magufuli alitangaza kumrejesha Tanzania kisha kumfutia hadhi ya Ubalozi.
Kukiwa na uvumi labda wa kutenda makossa ambayo yangemfanya kufikishwa kwenye vyombo vya sheria, hasa kutokana na kufutiwa hadhi ya ubalozi, tarehe 20 Septemba 2019, Hayati Magufuli akamteua Kidata kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Mtwara (RAS).
Nafasi hiyo ya RAS wa Mtwara, ameitumikia hadi Rais Samia amemteua tena kurejea kuongoza TRA.
Leave a comment