WAKATI Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kikiugulia maumivu ya kumpoteza Dk. Vicent Mashinji, aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, leo Boniface Mwambukusu ametimkia NCCR-Mageuzi. Anaripoti Kelvin Mwiapungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mwambukusu alikuwa mgombea Ubunge wa Jimbo la Busokelo (Chadema), Mbeya katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Mwanasiasa huyo ametangaza kujiunga na NCCR Mageuzi leo tarehe 19 Februari 2020, kwenye Mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho, uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Alipopata nafasi ya kueleza, Mwambukusu amesema uamuzi wake ni funzo kwa vijana kwamba siasa sio vyeo, bali ni kutanguliza mbele maslahi ya taifa.
“Bila kujali tuko kwenye mkutano, kama muwezeshaji lakini vile vile kwa leo nitaomba NCCR mkiona inafaa mnipokee, kwa nini tunafanya hivi? Tunataka kuonesha vijana, kwamba siasa sio vyeo, ni namna bora ya kutengeneza mazingira ya kuifanya Tanzania kuwa bora na salama na namna ya kuishi kuwa bora,” amesema Mwambukusu.
Mwanasiasa huyo amesema, amehamia NCCR-Mageuzi huku kukiwa na wimbi kubwa la wanachama wa Chadema kuhamia CCM, na kwamba haiwezekani watu wote wakavutiwa kukimbilia mahali kwa sababu ya kutafuta uharaka wa maisha.
“Hatuwezi kukimbilia sehemu moja kwa sababu ya kutafuta uharaka wa maisha, tunachotakiwa kufanya ni kujenga mfumo bora wa maridhiano ya kisiasa, maridhiano yenye kujenga utu, umoja na mshikamano wa kitaifa,” amesema Mwambukusu.
Leave a comment