KITUO cha Televisheni cha Tifu, Zanzibar kimefungiwa kwa siku saba baada ya kukiuka mwongozo wa vipindi wakati huu wa msiba wa Hayati Maalim Seif Sharif Hamad, aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais visiwani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Taarifa ya kufungia kituo hicho imetolewa leo Alhamis, tarehe 18 Februari 2021 na Omar Said, Katibu Mtendaji wa Tume ya Utangazaji Zanzibar ikieleza, tume hiyo imechukua uamuzi huo baada kituo hicho kurusha wa vipindi vyake kinyume na muongozo uliotolewa na tume hiyo.
Omar amesema, baada ya Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi kutangaza siku saba za maombolezo, tume ilitoa mwongozi wa vipindi katika siku saba za maombolezo kwa vituo vya televisheni, redio na mitandao ya kijamii.
https://www.youtube.com/watch?v=d8IvhpmTkI4
Amefafanua kuwa, mwongozo huo umeelekeza vyombo vya habari kubadili vipindi vyao na kuandaa vipindi maalumu vya maombolezo kwa siku saba.
Omar amesema, tume haikutaka kuchukua uamuzi huo lakini kwa kuwa Tifu kilikiuka mwongozo wa serikali, imelazimika kuchukua hatua hiyo.
“Iifahamike uamuzi huu umekuja kufuatia majadiliano ya vyombo vingine mbalimbali vya serikali, juu ya kitendo hicho, na ikaamuliwa kwa pamoja kichukuliwe hatua za kinidhamu,” amesema.
Leave a comment