TUNDU Lissu, mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ametoa hoja mbili za ‘kutojipeleka’ mbele ya Kamati ya Maadili ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC). Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Amesema, licha ya taarifa za kutakiwa kufika mbele ya Kamati ya Maadili ya NEC tarehe 2 Oktoba 2020, kusambaa kwenye mitandao ya kijamii, hatokwenda na ataendelea na tariba yake ya kampeni kama ilivyopangwa.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari leo tarehe 30 Septemba 2020, jijini Arusha amesema, mpaka muda huo akizungumza, hakuna ofisa yeyote aliyemfikishia ujumbe wa maandishi kumtaka afike kwenye kamati hiyo kama ambavyo kanuni zinaelekeza.
“Kama kweli mimi ni mlalamikiwa, kanuni za maadili zinasema mlalamikiwa huyo aandikiwe malalamiko na akabidhiwe, na pili: yeye ndiye anayetakiwa kuitwa. Sasa sijaona malalamiko yoyote, sijaona wito wowote. Kwa hiyo, mpaka sasa hakuna malalamiko yoyote,” amesema.
Amesema, malalamiko ama tuhuma zinazozungumzwa, amezisoma kwenye mitandao ya kijamii kama wengine walivyosoma kwamba, anatakiwa kufika mbele ya kamati hiyo tarehe 29 Septemba 2020 na baadaye ikabadilishwa na kuwa tarehe 2 Oktoba 2020.
“Nimesikia kulalamikiwa na kuitwa kwenye Kamati ya Maadili ya Uchaguzi ya Taifa. Mimi nimeona hizo taarifa mtandaoni kwamba kuna malalamiko kutoka CCM na NRA, kwamba nimekiuka kanuni za maadili ya uchagzi. Nilivyosomasoma nafikiri nilitakiwa kufika kwenye kikao cha maadili jana (tarehe 29 Septemba 2020).
“Baadaye nikaonaona taarifa kwamba natakiwa nifike kwenye kikao hicho tarehe 2 Oktoba, keshokutwa. Sasa, moja; kwa mujibu wa maadili ya uchaguzi na nakala ninayo hapa. Kama ni kweli kwamba, kuna malalamiko yoyote dhidi yangu kuhusiana na jambo lolote kwe nyeuchaguzi huu, malalamiko hayo ya maandishi yanatakiwa yaletwe kwangu.
“Mimi ndio mlalamikiwa basi mimi ndio natakiwa niletewe taarifa yoyote ya malalamiko hayo. Sijaona afisa yeyote wa tume ameniletea malalamiko yoyote, kuhusu jambo lolote,” amesema.

“Pili: Ili nijibu hizo tuhuma, ili niende kwenye kikao chochote cha tume, ninatakiwa niletewe mimi sio mtu mwingine yeyote, anayeletewa ni malalamikiwa, niletewe sio (kupelekwa) Makao Makuu ya chama, si mwenyekiti wa chama sio katibu mkuu, sio mtu meingine yeyote isipokuwa mimi. Hadi hapa niliposimama, sijaletewa wito wowote, wa kwenda popote nje ya ratiba yangu. ,” amesema.”
Amesema, NEC ilitoa kitabu cha maadili ya uchaguzi ambacho na wao wanapaswa kufuata yaliyomo kwenye kitabu hicho.
“Tume ina wajibu wa kufuata sheria, haipo juu ya sheria, hizi kanuni zimetengenezwa na tume yenyewe,” amesema.
Leave a comment