WATU wasiofahamika, wamefukua baadhi ya makaburi ya watu wenye Ualbino katika maeneo kadhaa nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa za karibuni kabisa zinasema, makaburi ya watu wawili wenye Ualbino mkoani Mbeya, mmoja wao akiwa amekufa mwaka 2015, mwili wake ulifukuliwa na baadhi ya mabaki kuchukuliwa na “watu wasiojulikana.”
Kaburi lililofukuliwa limetajwa kuwa ni la Aman Anywelwisye Kalyembe, ambaye alikufa mwaka 2015, wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya. Alikuwa ni mtu mwenye ualbino.
Katibu Mkuu wa chama cha watu wenye Ualbino nchini Tanzania (TAS), Mussa Kibimba amesema, “hatua ya watu kuvamia makaburi ya albino na kufukua miili ya marehemu, kumewafanya watu wenye ualbino kuishi kwa hofu.”
Kupatikana kwa taarifa ya kuibuka kwa vitendo vya kufua makaburi ya watu wenye ualbino na kuchukua baadhi ya sehemu ya viungo vyao, kumekuja siku tatu tangu mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea, kunukuliwa akisema anapanga kuwasilisha hoja binafsi bungeni, kutetea jamii hiyo.
Kubenea aliwaambia waandishi wa habari, Jumapili iliyopita, kwamba katika mkutano ujao wa Bunge, amepanga kuwasilisha hoja binafsi ili kushinikiza serikali kuridhia Itifaki ya pamoja ya Mkataba wa Afrika wa haki za binadamu, kuhusu haki za watu wenye Ualbino nchini.
Amesema, mkataba huo, uliyopitishwa na wakuu wan chi za Afrika katika mkutano wa 30 wa Umoja wa Afrika, uliofanyika Adis Sababa, Ethiopia, umelenga kulinda watu wenye ualbino.
Amesema, atatumia hoja yake hiyo, kutaka Bunge kuiagiza serikali kufanyia marejeo sera ya watu wenye ulemavu, ili ikidhi mahitaji ya makundi yote ya watu wenye ulemavu nchini.
Kwa mujibu wa Kubenea, mbali na watu wenye ualbino kufukuliwa makaburi yao, huuliwa kwa imani za kishirikina; na hukabiliwa na tatizo kubwa la saratani ya ngozi, uoni hafifu na kukatwa viungo.
Mpaka sasa, hakuna anayejua dhamira na dhumuni la wafukuaji wa makaburi mawili huko Mbeya; na wala hakuna anayejua masalio ya miili ya marehemu iliyofukuliwa imekwenda wapi.
Matukio haya ya kufukua makaburi yameleta hofu miongoni mwa albino na familia zao huku wengine wakidhani kuwa matukio hayo yanafanyika kwa sababu muda wa uchaguzi mkuu nchini humo umekaribia.
“Sisi ndio ni wahanga wakuu na tumepata misukosuko mingi. Tunaishi kwa hofu ya usalama wetu,” ameeleza Kibimba. Matukio ya kufukuliwa makaburi yalianza kuripotiwa mwaka 2016.
Tanzania ni miongoni mwa nchi za bara la Afrika lenye watu wengi wengi wenye ualbino nao hutambuliwa kutokana na rangi yao ya ngozi, macho na nywele zao.
Mauaji ya albino yalishamiri kutokana na matakwa ya waganga wa kienyeji ambao huwaambia wateja wao kwamba viungo vya Albino huleta bahati ya kupendwa, maisha marefu na mafanikio katika biashara.
Leave a comment