SAED Kubenea, Mbunge wa Ubungo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amesema atagombea tena jimbo hilo kupitia chama hicho, katika Uchaguzi Mkuu Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kubenea ametangaza uamuzi huo leo Jumamosi tarehe 13 Juni 2020 jijini Dar es Salaam, katika mkutano wake uliolenga kueleza aliyoyafanya katika kipindi cha miaka mitano kwa wadau wa jimbo la Ubungo.
Kubenea amesema muda wa uchukuaji fomu katika chama chake ukifika, atajitokeza katika kinyang’anyiro hicho.
Kubenea amesema, anaamini Kamati Kuu ya Chadema itampitisha tena kugombea jimbo hilo huku akisisitiza, hana mpango wa kuondoka katika chama hicho.
“Muda ukifika wa uchukuaji fomu katika Jimbo la Ubungo, nami nakusudia kuchukua na kugombea tena. Naomba mpuuze kauli za mitaani,” amesema Kubenea.
“Mimi niko Chadema, siondoki Chadema, nitagombea ubunge na naamini Kamati Kuu ya Chadema itanipitisha kwa sababu zilezile ilizotumia katika uchaguzi uliopita,” amesema Kubenea huku akishangiliwa na wadau waliojitokeza kumsikiliza.
Kauli hiyo ya msisitizo ya Kubenea kuhusu kutohama Chadema, imekuja kufuata tuhuma kadhaa kutoka kwa baadhi ya watu kwamba anataka kuondoka kwenye chama hicho na kugombea Ubunge kupitia chama kingine.
Leave a comment