MBUNGE wa Jimbo la Ubungo (Chadema), Saed Kubenea, amesema yupo tayari kuuza chochote alichonacho hadi afanikishwe operesheni ya kumwondoa ofisini Prof. Ibrahim Lipumba anayeng’ang’ania uenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) bila ridhaa ya wanachama, anaandika, Irene David.
Amesisitiza: “Azima ya kumwondoa msaliti Buguruni ipo palepale, na haiwezi kurejeshwa nyuma kwa maneno ya rejareja na ahadi za uongo au vitisho vya aina yoyote.
“Lipumba ni msaliti, na lazima aondoke. Na katika hili nitauza hata kiatu changu, lakini ataondoka.”
Wiki iliyopita, Kubenea, ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa Chadema, Kanda ya Pwani, aliwambia waandishi wa habari kuwa Chadema kimeamua kusaidia CUF katika jitihada za kumwondoa Lipumba kwenye ofisi anazokalia kimabavu Buguruni, Dar es Salaam.
Leo amemtaka Lipumba aache kusumbua jeshi la polisi ili lifanye kazi yake ya kupambana na uhalifu.
Lipumba anayebebwa na Msajili wa Vyama vya Siasa katika azima yake hiyo, juzi alikimbilia Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kumshitaki Kubenea, akidai mbunge huyo ametishia maisha yake.
Huku Lipumba akidai kwamba Kubenea amemtisha, mbunge huyo ameliambia Mwanahalisionline kuwa Lipumba amedhamiria kupotezea jeshi la polisi muda ambao lingetumia kufanya kazi zake za msingi.
Kubenea amekiri kupokea wito wa polisi kwa njia ya simu, akasema ataripoti kituoni kesho mchana, lakini akasisitiza kuwa hatayumba hadi ahakikishe wanafanikiwa kutimiza operesheni ambayo ameipa jina la Ondoa Msaliti Buguruni (OMB).
Kwa mujibu wa Kubenea, tayari matawi kadhaa ya CUF katika jimbo lake; na ambayo tayari yanaumga mkono operesheni hiyo.
Hadi kuuza kiatu! Kwa ajili ya kugharimia nini?
Wakati mwingine kuna watu ambao unadhani ni wazima lakini kumbe wana matatizo! Kubenea ni wa CHADEMA, ambacho kisiasa, kina misingi na wajibu wake katika kukiimarisha. Na mmoja ya misingi ya uimara wa chama ni kuwa na wanachama wengi pamoja na washabiki. Swali ni je, Kubenea anapambana na Lipumba ili achukue wanachama wake ili kuimarisha CHADEMA au anataka aifute CUF kwenye ukanda wake?
Aidha kwa nini anadhani kauli yake hii haina chembechembe za tishio la maisha kiasi cha kuona kama Prof. Lipumba anapoteza muda kwenda polisi? Alitaka Lipumba ashitakie kwa nani? Au alitaka iwe “jino kwa jino”?
Jitafakari!