MBUNGE wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea, ataendelea na ziara yake ya kikazi – kiserikali – ndani ya jimbo lake, kuanzia Jumatatu ya tarehe 6 Machi hadi tarehe 12 Machi 2017, anaandika Bupe Mwakiteleko.
Katika ziara hiyo, Kubenea atatembelea kata za Ubungo, Sinza, Kimara na Mburahati kwa lengo la kukagua shughuli za kiserikali kwa maana ya miradi ya maendeleo; kukutana na wananchi na kusikiliza kero zao; kuwafafanulia mambo mbalimbali yanayowahusu na baadaye kuhutubia mikutano ya hadhara.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na ofisi ya mbunge huyo, tarehe 6 Machi 2017, Kubenea atakuwa Kata ya Ubungo, tarehe 8 Machi (Jumatano), atakuwa kata ya Sinza, tarehe 10 Machi (Ijumaa), atakuwa Kata ya Kimara na tarehe 12 Machi (Jumapili), atakuwa Kata ya Mburahati.
“Hii ni awamu ya pili ya ziara ya Kubenea katika jimbo lake. Tayari ameshatembelea kata za Mabibo, Makuburi na Makurumla, ambako alikutana na wananchi na alihutubia mkutano wa hadhara,” imeeleza taarifa ya mbunge kwa wananchi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, ziara za mbunge huyo, zinatarajiwa kuanza kuanzia saa 5 asubuhi na kukamilika saa 10 jioni.
Leave a comment