MBUNGE wa Jimbo la Ubungo Saed Kubenea (Chadema) amewalipua Dk. Harrison Mwakyembe na Victor Mwambalasa kuwa ni miongoni mwa watu ambao wanahusika katika kupitisha mikataba feki ya madini kwa kwa faida zao binafsi, anaandika Dany Tibason.
Mbali na kuwataja watu hao kuwa ni wahusika katika kupitisha mikataba mibovu ya madini pia Kubenea amemtaka Rais John Magufuli kumtumbua Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Merdadi Kalemani kutokana na Naibu huyo kuwa mwanasheria wa Wizara hiyo.
Kubenea alitoa kauli hiyo leo bungeni wakati alipokuwa akichangia hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini ambayo inatarajiwa kupitishwa kesho.
Mbunge huyo amesema kwa sasa kitendo cha serikali kukamata mchanga bila kufuata sheria kinaweza kusababisha kuwepo kwa mkanganyiko mkubwa kibiashara, kidiplomasia na kimikataba, kwani mikataba ambayo imeingiwa na viongozi wengi wa serikali ya CCM ilikuwa mikataba isiyolinda rasilimali za nchi.
Amesema mwaka 1996 serikali ilipitisha mswada wa sheria wa kusafirisha dhaabu pamoja na kuruhusu mchanga kwenda kusafirishwa nje ya nchi pamoja na kuwaondolea kodi.
Amesema siyo kweli kuwa wapinzani wanapinga sakata la ukamatwaji wa makontena ya mchanga wa dhahabu na hakuna mbunge yoyote ambaye anataka mali za nchi ziibiwe na taifa liwe shamba la bibi.
Kubenea amesema ili kukabiliana na wizi wa dhahabu kwa sasa kunatakiwa kuwepo kwa mikakati ya uchunguzi wa kufika migodoni ambako mpaka sasa bado wizi wa madini unafanyika badala ya kukimbizana na mchanga wa dhahabu.
Amesema kuwa wapo viongozi wengi wa serikali ya CCM ambao wamehusika katika kusaini mikataba ya madini ambayo ina makosa mengi jambo ambalo limelisababishia taifa kukosekana kwa mapato ndani madini.
Akizungumzia kuhusu Naibu Waziri wa Nishati na Madini, anatakiwa kuondolewa katika nafasi yake kwani amekuwa mwanasheria wa Wizara ya Madini lakini bado anaendelea kushika nafasi yake ambayo kimsingi hastairi kuwepo.
Aidha alimtaka Waziri wa Fedha naye kuwajibika kwa kuwa Waziri wa Fedha ndiye mhusika mkuu wa kutoa misamaha ya kodi.
Leave a comment