SAED Kubenea, Mbunge wa jimbo la Ubungo, Dar es Salaam (Chadema) amejitoa kugombea nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Tanzania Bara. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Kubenea amewasilisha barua yake leo tarehe 16 Desemba 2019 kwa Katibu Mkuu wa Chadema, akidai ya kuwa Tundu Lissu, Mwanasheria Mkuu wa Chama hicho ambaye pia amejitokeza kugombea nafasi hiyo ataweza kufanya kazi ambazo angezifanya.
Akitangaza kujitoa kwa Mbunge huyo, John Mrema, Mkurugenzi wa Itifaki, Itikadi, Uenezi na Mambo ya Nje amesema kuwa chama kimepokea barua Kubenea kujitoa kwa ofisi ya msimamizi amble ni katibu mkuu.
“Asubuhi hii ndugu Saed Kubenea ameandika barua kwa Ofisi ya msimamizi ambaye ni Katibu Mkuu kuwa anajitoa katika kugombea nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa Chama Taifa hivyo Kamati Kuu imewapitisha Tundu Lissu na Sophia Mwakagenda kugombea nafasi hiyo Bara,” amesema.
Aidha amesema wakati Kubenea akiwasilisha barua ya kujitoa katika kugombea nafasi hiyo, chama hicho kimepokea rasmi barua ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, Frederick Sumaye ya kujitoa kwenye chama hivyo amepoteza sifa ya kugombea nafasi hiyo.
“Tumekuwa tukisikia sehemu mbalimbali Sumaye akitangaza kujitoa kwenye chama lakini leo tumepokea barua rasmi ya kujitoa kwake kwenye chama hivyo kwenye nafasi ya Uenyekiti Kamati Kuu imewateua Freeman Mboe na Cecil Mwambe kugombea nafasi ya uenyekiti taifa,” amesema.
Leave a comment