MBUNGE wa Ubungo, Dar es Salaam anayemaliza muda wake kupitia Chadema, Saed Kubenea amejiondoa ndani ya chama hicho na kujiunga na chama cha ACT-Wazalendo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
Kubenea amejiunga na ACT-Wazalendo leo Jumamosi tarehe 18 Julai 2020 na kupokelewa na Maalim Seif Sharif Hamad, Mwenyekiti wa chama hicho Kijitonyama jijini Dar es Salaam.
Pia, katika hafla hiyo, zaidi ya wanachama 48 wa Chadema wamejiunga na ACT-Wazalendo.
Mara baada ya kukabidhiwa kadi, Kubenea amemshukuru Maalim Seif kwa kumpokea.
“Nimekuwa kwenye harakati za kutetea mfumo wa vyama vingi, haki sawa kwa watu wote, haki za kisheria, haki za binadamu kwa karibu miaka 20 sasa. Nimekuwa mbunge wa Ubungo kwa miaka mitano,” amesema
Kubenea amesema, “nimelazimika kuondoka huko nilokokuwa. Nawashukuru sana viongozi wakuu bila kuwataka majina waliofanikisha mimi kufika leo.”
“Uamuzi huu haukuwa mwepesi, ulikuwa mgumu sana, kwa sababu katika maisha yangu, hiki ndicho chama cha pili kujiunga,” amesema mwandishi huyo wa habari
Kubenea amesema, “nilifika mahali nikasema, kama Maalim Seif alifika mahali akaondoka CUF aliyoianzisha. Mabere Marando mwasisi wa NCCR-M`ageuzi aliondoka na kujiunga na Chadema na wengine wengine, sembuse mimi.”
“Nilijifunza kwa wazee wangu hawa kwamba lazima safari ya mabadiliko iendelee. Nawashukuru sana wananchi wa Ubungo waliokuja kwenye chama chetu,” amesema
Kubenea amesema, katika Jiji la Dar es Salaam, upinzani una nguvu kubwa na kama vyama vya upinzani vikishirikiana vitafanya vizuri kuliko mwaka 2015 huku akiomba vyama hivyo kutanguliza maslahi ya wananchi mbele kuliko maslahi binafsi.
Leave a comment