MIRAJI Mtaturu ameapishwa rasmi kuwa Mbunge wa Singida Mashariki, akirithi mikoba ya Tundu Lissu aliyevuliwa ubunge wa Jimbo hilo. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Lissu alivuliwa ubunge kwa madai ya utoro na kutojaza fomu ya maadili ya umma.
Mtaturu ameapishwa leo tarehe 3 Septemba 2019 bungeni jijini Dodoma, siku moja baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kukataa ombi la Lissu la kuutaka mhimili huo kuzuia kuapishwa kwake, hadi pale shauri lake kuhusu kuvuliwa ubunge litakapotolewa uamuzi.
Mbele ya Bunge, Mtaturu alikula kiapo cha uaminifu, huku wabunge wa upinzani isipokuwa wa Chama cha Wananchi (CUF) wakisusia zoezi hilo kwa kutohudhuria bungeni.
Baada ya Mtaturu kuapa, Spika wa Bunge, Job Ndugai amewaomba wabunge wamkaribishe Mtaturu huku akieleza kwamba wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki wamepata mwakilishi halali bungeni.
“Kwa niaba yenu naomba tumkaribishe Miratji Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, sasa wananchi wa Singida Mashariki wanaye muwakilishi halali bungeni,” amesema Spika Ndugai.
Mnamo tarehe 28 Juni 2019 wakati akihitimisha mkutano wa kumi na tano wa Bunge, Spika Ndugai alitoa taarifa ya Lissu kuvuliwa ubunge Singida Mashariki.
Lakini tarehe 7 Agosti 2019 Lissu alifungua shauri Na. 18 la mwaka 2019 dhidi ya Spika wa Bunge na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) la kupinga kuvuliwa ubunge katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kwa hati ya dharula.
Leave a comment