VILIO na simanzi vimetawala Uwanja wa Uhuru mkoani Dar es Salaam, baada ya jeneza lenye mwili wa Hayati Rais John Pombe Magufuli kuwasili uwanjani hapo kwa ajili ya misa takatifu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mara baada ya msafara wenye mwili wa Dk. Magufuli kuwasili uwanjani hapo, vilio vilitawala uwanja mzima, si askari wa vikosi vya ulinzi na usalama au viongozi, walionekana wakibubujikwa machozi.
Jeneza lenye mwili wa Dk. Magufuli, wakati likiwekwa eneo maalum, Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliyekuwa kando, alionekana naye akibubujikwa na machozi.

Misa Takatifu ya kuuaga mwili wa Dk. Magufuli (61), inaongozwa na Askofu Mkuu wa Katoliki Jimbo la Dar es Salaam, Yuda Thadeus Ruwa’Ichi, akishirikiana na Askofu Mkuu Mstaafu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Father Charles Kitima.
Mwili wa Hayati Magufuli unatarajiwa kuagwa Dar es Salaam kwa siku mbili (Jumamosi na Jumapili), kisha tarehe 22 Machi 2021, mwili huo utaagwa katika Makao Makuu ya Nchi Dodoma.

Tarehe 23 Machi 2021, mwili wa Hayati Rais Magufuli utaagwa visiwani Zanzibar, kisha utasafirishwa Mwanza kwa ajili ya shughuli ya kuuaga tarehe 24 Machi 2021.
Baada ya kuagwa Mwanza, mwili wa Hayati Rais Magufuli utaagwa na wananchi wa Chato mkoani Geita, tarehe 25 Machi mwaka huu.
Baada ya mwili huo kuagwa Chato, shughuli za mazishi zitafanyika Ijumaa ijayo tarehe 26 Machi 2021, kijijini kwao Chato mkoa Geita
Leave a comment