KONGAMANO la kudai katiba mpya, lililoandaliwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), liko njia panda baada ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Robert Gabriel, kupiga marufuku mikusanyiko. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza…(endelea).
Kongamano hilo lilipangwa kufanyika kesho tarehe 21 Julai 2021, jijini Mwanza, baada ya kuzuiwa mara ya kwanza, tarehe 16 Julai mwaka huu.
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 20 Julai 2021, Gabriel amesema lengo la marufuku hiyo ni kudhibiti maambukizi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (Covid-19).
Mkuu wa mkoa huyo wa Mwanza, ameelekeza wilaya zote jijini humo, kutotoa vibali kwa matukio na mikusanyiko, aliyoita siyo ya lazima.
“Niendelee kusihi matukio ambayo sio ya dharura , sipendelei na nitoe wito kwa maneo ya wilaya zote, waangalie na wafanye tathimini. Kuna mambo ambayo naona sio ya lazima haina haja kuruhusu, ambayo yataleta madhara kwa watu bila sababu yoyote,” amesema Gabriel.
Aidha, Gabriel amewaeleza wageni waliopanga kwenda jijini humo kufanya matukio mbalimbali, kwamba mkoa huo uko katika kampeni ya kupambana na Covid-19.
“Nisihi tena kwamba, mikusanyiko isiyokuwa na sababu, kipindi hiki hatuna sababu ya kutoa vibali na niwatahadharishe hata wanaokuja Mwanza kwa ajili ya matukio makubwa, tuko kwenye kampeni kubwa,” amesema Gabriel.
Kongamano hilo la Chadema la kudai katiba mpya, lililoandaliwa na baraza la vijana la chama hicho (Bavicha), lilipangwa kufanyika Jumamosi iliyopita, lakini lilishindikana baada ya kukosa kibali.
MwanaHALISI Online ilimtafuta Mkurugenzi wa Itifaki na Mambo ya Nje Chadema, John Mrema, ili kujua hatma ya kongamano hilo, ambaye amesema chama hicho kitatoa tamko kuhusu suala hilo.
Hata hivyo, Mrema amesema “kiufupi yeye hajamtaka kwamba amezuia kongamano la katiba, sisi tunaandaa tamko tutalitoa baadae.”
Leave a comment