Kampuni ya vinjwaji Baridi ya Coca Cola kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Dunia (FIFA), linatarajia kulileta nchini kombe la Dunia kwa ziara ya siku mbili kuanzia Tarehe 31 Mei 2022. Anaripoti Mwamdishi Wetu…(endelea)
Kombe hilo linashuka nchini Tanzania kwa mara ya pili, kabla ya kuelekea nchini Qatar ambapo michuano hiyo kwa mwaka huu itatimua vumbi kuanzia mwezi Novemba.
Hafla ya utambulishwaji wa ziara hiyo, imefanyika hii leo jijini Dar es Salaam, na kuhudhuliwa na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohammed Mchengerwa, rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia sambamba na mwenyeji wao ambaye ni mkurugezni mkuu wa Coca Cola Unguu Sulay.
Katika hafla hiyo mkurugenzi mkuu wa kampuni hiyo, alitabaisha kuwa ziara hiyo ni muendelezo wa kampuni yao kurudisha kiu na mipango ta Tanzania katika kusaka tiketi ya kushiriki kwa mara ya kwanza fainali hizo katika miaka ya baadaye.
“Sio kila Taifa linapata hii nafasi,Tanzania imekuwa ni tofauti tumepata nafasi hii kwa mara ya nne kulipokea kombe hili halisi na watu kupata nafasi ya kupiga nalo picha,” alisema Sulay.
Tanzania ni moja ya nchi tisa ambazo kombe hilo lenye thamani kubwa ulimwenguni litapita, kwa ajili ya kuhamasisha maendeleo na ukuaji wa mchezo wa mpira wa Miguu.
Aidha Mkurugezni huyo aliendelea kusema kuwa, kombe hilo litakaa nchini kwa siku mbili kabla ya kwenda nchini Qatar, kwenye michuano hiyo itakayonza kutimua vumbi Novemba mwaka huu.
“Kombe hili litakuwa hapa nchini kwa siku mbili kuanzia Mei 31 na Juni Mosi na huu ni muendelezo wa kampuni yetu sio tu kuishia kuburudisha kupitia vinywaji bora lakini pia kujihusisha na moja kwa moja na msisimko wa kimichezo kupitia soka na burudani.
Kwa upande wa Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohammed Mchengerwa, ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye hafla hiyo alisema kuwa, robo tatu ya Watanzania wanapenda michezo na ziara hii inakuja kuwapa fursa watu wengi wenye rika tofauti kushuhudia kombe hili ambalo Tanzania inafanikisha ndoto za kuandaa fainali hizi.
“Serikali na wizara yetu ya michezo imefarijika na ziara hii ikiwezeshwa na ninyi Coca cola, Rais wetu (Samia Suluhu Hassan) anapenda michezo na tuna ndoto za siku moja tuje kuandaa fainali hizi ingawa kwanza tunatakiwa kuamini inawezekana na baada ya hapo tujenge miundo mbinu kama vile viwanja,” alisema Mchengerwa….
Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Wallace Karia alisema ziara hii ya kombe hili ni muendelezo wa ushirikiano bora kati ya kampuni hiyo na TFF katika maendeleo ya mpira.
” Coca cola imekuwa na mkono mzuri katika kuendeleza soka, sijui kama watu wanafahamu timu yetu ya Taifa Stars ya sasa ina wachezaji wengi ambao walizalishwa na mkakati wa kuzalisha vijana uliodhaminiwa na kampuni hii na ukaleta matunda bora kwa Taifa letu,”alisema Karia.
Hii ni mara ya pili kwa kombe hilo kuja nchini, ikumbukwe mara ya mwisho kombe hilo lilikuja Novemba 13, 2013 jijini Mwanza na kupokelea na Rais mstaafu wa awamu ya nne Jakaya Mrisho Kikwete
Leave a comment