KODI ya mitandao ya simu imeibua mjadala, baada ya kupingwa kila kona na baadhi ya watu, kwa maelezo kwamba itaumiza wananchi hasa wasiokuwa na kipato cha kutosha.Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kodi hiyo iliyopewa jina la ‘Mshikamano’, imeanza kutozwa leo Alhamisi, tarehe 15 Julai 2021, baada ya kupitishwa na Bunge la Bajeti, lililohitimisha shughuli zake hivi karibuni.
Kwa mujibu wa kodi hiyo ya miamala ya simu, mtumiaji anatozwa kuanzia Sh. 10 hadi 10,000, katika muamala wa kutuma au kutoa pesa, kulingana na thamani ya muamala wa fedha husika.
katika mjadala huo, Baraka Mchau, ameishauri Serikali ipunguze mishahara na posho za mawaziri na wabunge, ili ipate fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo, badala ya kuwakamua wananchi.
“Hivi kwa nini mishahara pamoja na posho za wabunge na mawaziri zisipunguzwe ili kufidia makato na gharama za kodi ya mshikamano,” ameandika Mchau katika mtandao wa Twitter.
Mchau alitoa ushauri huo, akitoa maoni yake kwenye ukurasa wa Twitter wa Mwanaharakati Maria Sarungi, aliyetangaza kuandaa kikao cha mtandaoni, kwa ajili ya kujadili athari za makato hayo.
Kikao hicho kinatarajiwa kufanyika kesho tarehe 16 Julai 2021, katika programu ya Space, inayopatikana kwenye mtandao huo, huku Katibu Mkuu Baraza la Wanawale la Chadema (Bawacha), Catherine Ruge, akitarajiwa kuwa miongoni mwa watoa mada.
Naye Samwel Mafwele, ametoa maoni yake akisema katika mtandao huo akisema “yaani ilitakiwa mahakama iingilie kati mpaka sasa.”
Eric Boniface, naye amechangia katika mjadala huo akisema, tozo hizo zinakwenda kinyume na malengo ya uanzishwaji wa huduma za fedha mtandaoni.
“Teknolojia hii haikuanzishwa kwa ajili ya kuwakamua wananchi, bali kuwapunguzia gharama za utumaji, upokeaji wa fedha na muda. Uamuzi wa Serikali wa tozo ya mshikamano unakwenda kinyume na lengo la teknolojia hii,” ameandika Boniface.
Hata hivyo, Adam Adam, ametofautiana na wachangia mjadala huo akisema, kodi ndiyo inafanikisha nchi nyingi kupiga hatua za kimaendeleo.
“Nchi nyingi za ulimwengu wa kwanza, ndizo zinazoongoza kwa ulipaji kodi. Suala si kodi ya nini, tunanachohitaji hizo kodi wanazotufanya tulipe ziwe na matokeo chanya,” amechangia Adam.
Serikali ya Tanzania inatarajia kutumia zaidi ya Sh. 600 bilioni, fedha zitakazotokana na kodi hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2021/22, kwa ajili ya utekelezaji miradi ya elimu, afya ya msingi na miundombinu ya barabara.
Kwa mujibu wa Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Ummy Mwalimu, fedha hizo zitatumika kujenga vyumba vya madarasa zaidi ya 10,000, maabara za sayansi za shule za sekondari 1,043, shule za kata 300 na shule za sayansi za sekondari za wasichana 10.
Pia, zitatumika kujenga zahanati 756 na kukamilisha maboma ya zahanati 900, pamoja na kununua vifaa tiba.
Kwa upande wa miundombinu, fedha hizo zinatarajia kujenga barabara za kiwango cha lami zenye urefu wa kilomita 250, kupandisha hadhi barabara za udongo kuwa changarawe urefu wa kilomita 5,834 na madaraja makubwa 64.
Leave a comment