KOCHA wa Simba ya Dar es Salaam, Didier Gomes amesema, mchezo wao dhidi ya Al Merrikh ya Sudan, utakuwa mgumu lakini “lazima tushinde.” Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Simba itacheza na Al Merrikh, kesho Jumanne, tarehe 16 Machi 2021, kuanzia 10:00 jioni, katika Uwanja wa Benjaim Mkapa, Dar es Salaam, nchini Tanzania.
Utakuwa mchezo wa marudio kwa timu hizo, kwenye michuano ya klabu Bingwa Afrika, ukitanguliwa na ule wa awali, uliochezwa wiki mbili zilizopita, nchini Sudan na kutoka sare ya bila kufungana.
Leo Jumanne, kocha wa Simba, Gomes akizungumzia mchezo huo amesema, “lazima tushinde, ni muhimu sana kupata alama tatu kesho sababu kwenye hili kundi ili kufika robo fainali tunahitaji alama 11, hivyo ni muhimu sana kushinda. Kwa nilichokiona kwenye mazoezi kwa siku hizi tupo vizuri.”
Simba inaongoza kundi A la michuano hiyo ikiwa na pointi saba. Timu zingine kwenye kundi hilo ni As Vital ya Congo na Al Ahly ya Misiri, ambazo zote zina pointi nne kila mmoja huku Al Merrikh ikishika mkia kwa kuwa na pointi moja.
Kocha Gomes amesema, kwenye mchezo huo, beki wao kisiki, Paschal Wawa ataukosa kutokana na kuwa majeruhi, “lakini tunao wachezaji wengine wazuri ambao wanaweza kucheza nafasi yake.”
Amegusia suala la kutokuwapo kwa mashabiki kwenye mchezo huo akisema, wamejiandaa vyema kuhakikisha mwisho mwa mchezo, mashabiki wao popote watakapokuwa wanakuwa na furaha kutokana na ushindi watakaokuwa wameupata.
Kwa upande wake, Nahonda wa timun hiyo, John Bocco amesema, wamejiandaa kucheza bila mashabiki na kuwaomba popote pale walipo kuwaombea ili kuwawezesha kuibuka na ushindi.
Leave a comment