KOCHA mkongwe nchini, Joseph Kanakamfumu ambaye pia amewahi kuwa Mkurugezni wa Michezo wa Chama cha Mpira wa Miguu mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) amempigia chapuo aliyekuwa kocha wa Taifa Stars, Etienne Ndayilagije kuchukua mikoba ya Cedric Kaze ndani ya Yanga. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kaze alitimuliwa jana kufuatia mlolongo wa matokeo mabovu waliyoyapata klabu hiyo kwenye michezo sita ya Ligi Kuu Bara, muda mchache baada ya kutoka sare ya mabao 1-1 dhidi ya Polisi Tanzania.
Akiongea na Mwandishi wa MwanaHalisi Online kwa njia ya simu na kuulizwa swali kuwa Je ni kocha wa aina gani ambaye atawafaa Yanga kwa sasa? Kanakamfumu amesema kuwa Etiene Ndayilagije atawasaidia sana.
“Mimi ni mwalimu na ningekuwa upande wa uongozi ni lazima tutafute kocha na bila kupepesa macho Etienne Ndayilagije angewasaidia sana tena akishirikiana na Mecky Maxime ni vichwa viwili vinavyoweza kufanya kazi nzuri,” alisema mkongwe huyo.
Ndayilagije ambaye alikuwa kocha mkuu wa kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) alitimuliwa mwezi mmoja uliopita na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kufuatia matokeo mabovu ya timu hiyi kwenye michuano ya CHAN.
Michezo sita ya Ligi Kuu Tanzania Bara ilitosha kumuondoa Cedric Kaze mara baada ya kupata ushindi katika mechi moja, akipoteza mmoja na kwenda sare mechi nne na kuonekana kutowafurahisha mabosi wa Yanga na kuamua kuachana naye.
Leave a comment