KOCHA wa klabu ya Mbeya Kwanza inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara, Mbwana Makata pamoja na meneja wa kikosi hiko David Naftari wamefungiwa miaka mitano kila mmoja kufuatia kuwashawishi wachezaji wao kugomea mchezo wao dhidi ya Namungo FC. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mchezo huo namba 180, kati ya Namungo dhidi ya Mbeya Kwanza ulishindwa kufanyika kufuatia klabu ya Mbeya kwanza kugomea mchezo kwa kigezo cha kutokuwepo Uwanjani kwa gari la kubebea wagonjwa (Ambulance) kanuni ya 17 inavyoeleza.
Gari hilo lilikuja Uwanjani kwa kuchelewa kwenye majira ya saa 10:24, lakini benchi la ufundi la klabu hiyo ya Mbeya Kwanza halikuingiza timu uwanjani kwa kigezo cha muda kupita.
Mara baada ya mchezo huo, kamati ya uendeshaji na usimamizi wa Ligi (kamati ya saa 72), katika kikao chao, waligundua kwamba viongozi hao walifanya makosa kiasi cha kuwachukulia hatua hizo.
Aidha katika hatua nyingine kamati ya saa 72 iliwapa ushindi klabu ya Namungo wa alama tatu na mabao matatu, kufuatia klabu ya Mbeya Kwanza kufanya kosa hilo la kikanuni.
Klabu hiyo imekosa alama tatu huku ikiwa ya mwisho kwenye masimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, ambayo imebakisha michezo saba kuelekea ukingoni.
Leave a comment