KUELEKEA mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya klabu ya Simba, kocha mkuu wa kikosi cha Biashara United Vivie Bahati, amefunguka kuwa wanakikosi imara kitakachoweza kukabiliana na Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mchezo huo wa mzunguko wa pili, utapigwa kesho majira ya saa 1 usiku, kwenye dimba la Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.
Akizungumza mbele ya waandishi wa Habari leo Alhamis Tarehe 3 Machi 2022, kocha huyo alisema kuwa mpaka sasa kikosi chake kipo kamili na hakina majeruhi yoyote na wap[o tayari kwa mchezo huo.
“Niseme tu, timu tunayo mpaka sasa hatuna majeruhi wala aliyefungiwa kwa ajili ya kadi na timu ipo vizuri”.
“Kesho itakuwa mechi nzuri, tumefanya maandalizi vizuri, naamini tutapata matokeo mazuri”. Alisema kocha huyo
Simba inarejea kwenuye michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara, mara baada ya kutoka kucheza michezo miwili kwenye michuano ya kombe la Shirikisho Barani Afrika.
Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, walitua nchini siku ya Jumanne Machi Mosi, 2022 wakitokea nchini Morocco kwenye mchezo wa kundi D, dhidi ya Berkane ambapo walipoteza kwa mabao 2-0.
Licha ya kufunguka kuwa wana kikosi cha kupambana na Simba, Bahati alikili kwamba kwa sasa Simba ina timu bora kutokana na ushiriki wao kwenye michuano ya kimataifa lakini wao wamejipanga kuondoka na alama tatu.
“Kwanza tunajua ubora wa simba, kiwango chao kipo juu wametoka kimataifa wamefanya vizuri, kesho lazima tujilinde na tukipata tutacheza ila malengo ni kupata alama tatu”. Alisema kocha huyo
Katika mchezo wa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Biashara United walifungua pazia hilo kwa kumenyana na bingwa huyo mtetezi kwenye mchezo ulipigwa kwenye Dimba la Nelson Mandela mkoani Rukwa na timu hizo zikaenda sare ya bila kufungana.
Leave a comment