Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Elsewedy Electric East Africa Ltd kwa ukanda wa Afrika Mashariki, Mhandisi Ibrahim Qamar amesema katika awamu ya kwanza ya ujenzi wa kiwanda hicho wameajiri Watanzania 500 lakini ujenzi wake utakapokamilika kitaajiria watu 1,000. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mkurugenzi huyo ametoa kauli hiyo leo tarehe 6 Disemba jijini Dar es salaam wakati akizungumza katika uzinduzi rasmi wa kiwanda hicho ambao umeongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.
Amesema kiwanda hicho cha utengenezaji wa nyaya za umeme, transfoma na vifaa vingine vya umeme kilianza kama kama kiwanda cha familia mwaka 1938 huko nchini Misri na kukua kufikia ngazi za kimataifa.
“Kiwanda kinazalisha nyaya, transfoma za voltage za chini, kati na juu. Awamu ya kwanza tulitumia Dola za Marekani milioni 40 na kuanza uzalishaji Tanzania mwaka 2020,” amesema.
Amesema mkakati wa kiwanda hicho ni kujielekeza zaidi kujenga uwezo, kutoa mafunzo kwa wafanyakaz.
“Tunayofuraha kuwakaribisha wafanyakazi Watanzania 18 waliotembelea kiwanda chetu Misri. Walikaa mwezi mzima na kupata mafunzo kazini na hao ndio wanakuwa kiini cha uzalishaji Tanzania,” amesema
Amesema kiwanda hicho kitakuwa kituo cha kikanda upande wa Afrika Mashiriki na Kusini mbali na kuhudumia Tanzania.
Aidha, Rais na Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hiki, Mhandisi Ahmed El Sewedy ameongeza kuwa wanafanya kazi katika nchi mbaliambali duniani ikiwamo Barani Afrika na ukanda wa Ghuba.
Hata hivyo, ameishukuru Serikali kwa heshima waliyoipata ya kushirikiana na kampuni ya Arab Contractors kujenga Bwawa la uzalishaji umeme wa maji la Mwalimu Nyerere ambalo ujenzi wake unaendelea huko Rufiji mkoani Pwani.
“Tunaahidi kuwa tutafanya kazi nzuri katika bwawa hilo ambalo litawasaidia Watanzania wengi kupatika umeme wa uhakika, kuzalishaji wa ajira na kuboreshaji yao.
“Tangu tulipokutana na Rais Samia miezi miwili iliyopita tulimuahidi kuwa tutaongeza zaidi uwekezaji Tanzania na tutaifanya kuwa nchi yetu ya pili katika uwekezaji kutoka Misri,” amesema.
Amesema baada ya kufika nchini na ujumbe wa wawekezaji mbalimbali nchini siku mbili zilizopita, wamefurahia mazingira ya uwekezaji nchini baada ya kupokewa vizuri.
“Tunaamini ndani ya mwaka mmoja utaona namna uwekezaji wetu utazalisha ajira, kutoa mafunzo kwa ajili ya ufundi mchundo na ufundi stadi katika kuhakikisha Watanzania wanapata na ajira na maisha bora,” amesema
Aidha, naye Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Assem El Gazzar ambaye aliongoza ujumbe wa uwekezaji kutoka Misri amesema ni furaha kupata mapokezi hayo ya kipekee nchini.
Amesema ujumbe huo wa wawekezaji pia umekuja kutembelea maendeleo ya ujenzi wa mradi wa bwawa hilo la umeme kwa maagizo ya Rais wa Misri, Abdel Fattah al-Sisi.
Amesema ndani ya kipindi cha miaka mitatu wamekuwa wakitoa taarifa ya maendeleo ya mradi huo kila mwezi kwa Rais huyo wa Misri ili kuhakikisha kila kitu kinaenda kama kilivyopangwa.
“Niwahakikishie kwamba mradi huu unaotekelezwa na kampuni ya Elsewedy kwa kushirikiana na Arab Contructors utakamilka kwa manufaa ya Watanzania na kufikia kuwa sehemu ya nchi inayoongoza kwa uzalisha wa umeme Afrika,” amesema.
Leave a comment