RAIS wa Tanzania, John Magufuli amezindua Daraja la Juu la Ubungi na Kituo cha Mabasi yaendayo mikoani na nje ya nchi, Mbezi Luis jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Uzinduzi huo umefanyika leo Jumatano tarehe 24 Februari 2021, , akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu jijini humo.
Rais Magufuli ameliita daraja hilo la Kijazi ili kutambua utumishi uliotukuka wa aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Mhandisi John Kijazi ambaye alifariki dunia tarehe 17 Februari 2021.
Balozi Kijazi, alifikwa na mauti akiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu na tayari mwili wake, umezikwa nyumbani kwao, Korogwe mkoani Tanga.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Rais Magufuli amesema daraja hilo lililopewa jina la ‘Daraja la Kijazi’ litasaidia kupunguza foleni jijini humo, na kuwataka Watanzania kulitunza.
Amesema, daraja hilo limejengwa kwa fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia (W.B) na kwamba zitalipwa na wananchi wa Tanzania.
“Daraja lipo, tumebaki na deni ambalo linaanza kulipwa mara moja, ndio maana nasema hili ni la Watanzania, sababu fedha zilizojenga hapa ni za Watanzania watakaolipa, nashukuru benki ya dunia kwa kukubali kutukopesha, na nawashukuru Watanzania waliokubali kulipa deni kwa manufaa ya nchi,” amesema Rais Magufuli.
Awali, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Mhandisi Patrick Mfugale amesema, daraja hilo limejengwa kwa gharama ya Sh.229.8 bilioni, ambazo ni mkopo kutoka Benki ya Dunia, huku Serikali ya Tanzania ikitoa Sh.8.375 bilioni kwa ajili ya kulipa fidia wananchi.
Mhandisi Mfugale amesema, mkandarasi aliyejenga daraja hilo, China Civil Engineering Company ameshalipwa Sh.152 bilioni.
Kuhusu Kituo cha Mabasi ya Mbezi Luis, kilichopewa jina la Kituo cha Mabasi Magufuli,’ Rais Magufuli ameagiza wafanyabiashara wadogo (machinga), wasikatazwe kufanya biashara katika stendi hiyo.
“Wamachinga wasifukuzwe, muwatengenezee utaratibu , sababu kama mabasi 3,000 watapakia abiria. Hao abiria wakanunue chakula kwa wamachinga, wenye hela nyingi waende kwenye hoteli, lakini mihogo ya mama lishe nayo inunuliwe. hiyo ndio itakuwa serikali inayojali wananchi wake,” ameagiza Rais Magufuli.
Akitoa taarifa za mradi wa kituo hicho, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Tamisemi, Mhandisi Joseph Nyamhanga amesema, umegharimu Sh.50.947 bilioni, fedha zilizotolewa na Serikali ya Tanzania na kwamba hadi sasa Serikali imeshalipa Sh.34 bilioni
Mhandisi Nyamhanga amesema, kituo hicho kina uwezo wa kubeba magari 3,456 kwa siku, magari madogo 280 kwa wakati mmoja na kuhudumia abiria 224,640.
Leave a comment