KITENGO cha kudhibiti fedha haramu nchini Tanzania kimeelemewa na miamala iliyotiliwa mashaka ambayo inatakiwa kufanyiwa uchunguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamebainishwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Omary Kigua, leo Jumanne tarehe 7 Juni, 2022 bungeni jijini Dodoma, akiwasilisha taarifa ya kamati kuhusu bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango yam waka 2022/23.
Kigua amesema hadi mwezi Aprili, 2022 kitengo kilikuwa kimepokea taarifa ya jumla ya miamala Shuku 12,840.
Amesema kati ya miamala hiyo miamala 2,186 ilihusu usafirishaji wa fedha kutoka na kuingia nchini; Miamala 5,251 ilihusu fedha taslimu, Miamala ya 5,403 ilihusu kutuma fedha kwa njia ya kielektroniki.
“Jambo ambalo linasikitisha ni kwamba miamala ambayo uchunguzi umekamilika na kuwasilishwa taarifa zake fiche za fedha kwa vyombo vinavyosimamia utekelezaji wa sheria ni 101 tu sawa na asilimia 0.78,” amesema Kigua katika taarifa hiyo.
Amesema “madhara yake ni fedha za wananchi kuendelea kushikiliwa katika mabenki na Taasisi za fedha na hivyo kuleta taharuki.”
“Kamati inaishauri Serikali kuhakikisha kwamba kitengo hikii kinawezehswa kifedha na rasilimali watu ili kuondoa taharuki hiyo.”
Aidha Kamati imeshauri Serikali kuanzishwa kwa Mamlaka kamili ya kudhibiti fedha haramu ili iweze kufanya kazi hiyo kwa ufanisi.
“Ili kifanye kazi kwa ufanisi Kitengo kipewe hadhi ya kuwa Mamlaka kamili kuliko kilivyo sasa ambapo asilimia 90 ya watumishi wake ni wa kuazima kutoka mafungu na taasisi zingine,” amesema.
Leave a comment