SERIKALI ya Tanzania imetangaza kusudio la kutumia Kiswahili katika kufanya usaili wa watumishi umma. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea)
Mwigulu ametangaza mapendekezo hayo leo Jumanne tarehe 14 Juni 2022 bungeni jijini Dodoma akiwasilisha bajeti kuu ya Serikali kwa mwaka 2022/23.
Waziri huyo amesema lugha ya kiswahili “ndio lugha ya Taifa, ndio lugha ya ofisini, ndio lugha ya pili kwa watoto wa vijijini na lugha ya kwanza kwa watoto waliowengi wa sasa, ndio lugha ya msingi, ni lugha ya Bunge, na nikiwa Waziri wa Katiba na Sheria nilileta mapendekezo kuifanya kuwa lugha ya Mahakama na lugha ya hukumu.”
“Hii ndiyo lugha yetu, kwa nini usaili wa mtoto wa kitanzania anapotafuta kazi unafanyika kwa lugha ya Kingereza?” amehoji Dk. Nchemba na kuongeza;
“Yaani afisa kilimo, afisa mifugo, mtumishi wa Serikali anakazi ya kuhudumia watanzania tunapima akili zake kwa kupima kingereza chake kwa ajili ya nini? Ameendelea kuhoji.
“Napendekeza saili zote zifanyike kwa Kiswahili, na kumbi zote za mikutano na ofisi za Serikali ziwe na vifaa vya kutafsiria lugha za kigeni na watafsiri ili tuweze kuienzi lugha yetu ya Taifa,” amesema.
Amesema Kiswahili ni lugha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) “ambapo tumeipeleka wenyewe, ikiwa ni pamoja na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Umoja wa Afrika (AU).
Vilevile, amesema UNESCO wameitambua na watakuwa wanaiadhimisha tarehe 7 Julai kila mwaka.
Leave a comment