VIONGOZI kutoka nchi za Ufaransa, Marekani na Urusi wanazuru bara la Afrika, katika kile kinachoelezwa ni kuyashawishi mataifa ya Afrika kuunga misimamo yao kuhusu vita vinavyoendelea nchini Ukraine. Anaripoti Juliana Assenga, (UDSM)… (endelea).
Hatua hii pia inaelezwa kama ushindani mkubwa wa mataifa hayo kuwahi kushuhudiwa barani Afrika, tangu wakati wa vita baridi.
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amekuwa katika nchi za Cameroon, Benin na Guinea Bissau huku akiishtumu Urusi kama mkoloni anayesalia duniani.
Pia amewakosoa pia viongozi wa mataifa ya Afrika kwa kutoonesha msimamo thabiti wa kusimama na Ukraine na kuilaani Urusi kwa uvamizi unaoendelea.
Aidha, ameishutumu Urusi kwa kutumia vyombo vyake vya Habari kwa kueneza Habari za propaganda kuhusu vita vnavyoendelea nchini Ukraine.
Naye, Waziri wa Mambo ya nje wa Urusi, Sergey Lavrov ambaye amekuwa nchini Misri, Congo Brazavile, Uganda na Ethiopia ameyashtumu mataifa ya Magharibi kwa kuchochea mzozo kati yake na Ukraine.
Pia ameitetea nchi yake dhidi ya shutuma za kusababisha kupanda kwa gharama ya vyakula duniani.
Samantha Power, Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo nchini Marekani naye alikuwa nchini Kenya na Somalia wiki iliyopita.
Pia balozi wake kwenye Umoja wa Mataifa Linda Thomas-Greenfield, anatarajiwa kuzuru Ghana na Uganda wiki ijayo katika kile kinachoelezwa ni kuendeleza ushawishi kwa mataifa ya Afrika.
Leave a comment