RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amemwagiza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuunda kamati ya kwenda kuchunguza mauaji yaliyotolea mkoani Mtwara yanayodaiwa kufanya na Jeshi la Polisi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Mauaji hayo ya mfanyabiashara wa madini, aliyefahamika Mussa Hamis Hamis, maarufu “Mussa Dola,” yanadaiwa kufanywa na jeshi ka polisi baada ya kuporwa Sh. 70 milioni na kisha kuuawa kwa kuchomwa sindano ya sumu na baadae mwili wake kuutupa baharini, zinadizi kufichuka.
Taarifa zinasema, maofisa saba wa polisi wanaotuhumiwa kutekeleza tukio hilo wamekwisha pandishwa kinzimbani kujibu tuhuma za mauaji hayo yanayodaiwa kutokea tarehe 15 Januari 2022.
Aidha, Afisa mwingine wa Polisi, Inspekta Msaidizi wa Polisi, Grayson Gaitan Mahembe, anadaiwa kujinyonga 22 Januari 2022 akiwa mahabusu ya Polisi, mkoani Mtwara akidaiwa kutumia tambala za deki.
Leo Ijumaa, tarehe 4 Februari 2022, akiwa njiani kutoka Mwanza kwenda mkoani Mara kwenye ziara ya siku nne, amezungumza na wananchi na kugusia matukio hayo ya mauaji. Jeshi la Polisi linaaongozwa na Simon Sirro.
Ni baada ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Yusuf Masauni kumaliza kuzungumza na wananchi wa Mwanza na kukemea mauaji yanayoendelea, Rais Samia alisema, “kuna mauaji yametokea Mtwara na kwa taarifa zilizopo ni jeshi lako ndilo limefanya mauaji.”
“Kwa maana hiyo, taarifa niliyonayo jeshi limetengeneza kamati ya kufuatilia mauaji hayo, haiwezekani jeshi lifanye mauaji, jeshi lichunguze lenyewe,” alisema Rais Samia huku akishangiliwa na wananchi.
Mkuu huyo wa nchi alisema “ndugu zangu wananchi na Watanzania, nimemwelekeza waziri mkuu (Kassim Majaliwa) aunde kamati nyingine iende kufanya uchunguzi wa mauaji yaliyofanywa na jeshi la polisi, halafu watuletee taarifa lakini wakati huo huo, Waziri Masauni nataka jeshi lako lijitafakari wanaone kama kinachotokea ndio misingi ya jeshi la polisi au vinginevyo.”
“Tunasubiri taarifa itakayoundwa na waziri mkuu ituletee ripoti, tulinganishe na ya jeshi la polisi na tuone taarifa mbili zinasemaje na tuchukue mwafaka,” alisema.
Amiri Jeshi Mkuu huyo aliwaomba wananchi kutunza amani kwani matukio ya uhalifu yanapoongezeka serikali inaelekeza nguvu kuyashughulikia kuliko kujikita kuwapelekea wananchi maendeleo.
Leave a comment