NDOA tamu! Eeh… ndivyo ‘couple’ moja huko nchini India ilivyothibitisha kuwa kilichohalalishwa na Mungu mwanadamu hawezi kukipinga baada ya kuwasili salama kanisani kwao katika siku ya ndoa yao kwa kutumia usafiri wa sufuria. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hatua hiyo imekuja baada barabara waliyokuwa wakitumia wapenzi hao kuelekea kanisani kwao katika mji jirani, kujaa maji kutokana na mvua kubwa zilizonyesha mfululizo kuanzia wiki iliyopita na kusababisha maafa na kuharibu miundombinu katika jimbo la kusini la Kerala nchini humo.
Katika picha zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha wawili hao Akash Kunjumon na Aishwarya wakiwa ndani ya sufuria kubwa ya kupikia huku wanaume wawili na mpiga picha mmoja wakiisukuma sufuria hiyo iliyokuwa inaelea kwenye maji.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini humo, wanandoa hao walikodisha sufuria hiyo kutoka katika kanisa moja kwa kuwa ndio njia pekee iliyokuwa imebakia kufika katika eneo la kufungia ndoa hiyo.
Licha ya mvua hiyo kubwa iliyosababisha maporomoko na mafuriko yaliyoua watu 27, wawili hao hawakukata tamaa wala kuahirisha siku yao hiyo kubwa na ya kipekee.
Aidha, picha zinaonesha kuwa wapenzi hao waliwasili salama tena bila kuloa maji katika kanisa walilopanga kufungia ndoa lililopo katika mji wa Thalavady, kisha kubadilisha maua kama ishara ya ndoa kwa mujibu wa tamaduni za Kihindu.
“Imegeuka kuwa harusi ambayo hatukuwahi kuifikiria,” Bi harusi Aishwarya aliambia kituo cha habari Asianet.
Wawili hao ambao sasa rasmi ni mume na mke wote ni watabibu katika hospitali moja katika mji wa Chengannur nchini humo.
Leave a comment