KASSIM Majaliwa, Waziri Mkuu wa Tanzania, amebainisha mambo saba ambayo wananchi wanapaswa kuyazingatia ili kuchungua tahadhari ya kujikinga na maambukizi ya corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Miongoni mwa mikakati hiyo ni “kusitisha safari za ndege zetu kwenda katika mataifa yaliyoathirika kwa kiasi kikubwa.”
Majaliwa amesema hayo leo Jumatano, tarehe 30 Juni 2021, wakati akitoa hotuba ya kuahirishwa kwa mkutano wa tatu wa Bunge hilo, lililoanza vikao vyake 30 Machi 2021.
Hoja hiyo iliungwa mkono na Bunge na sasa Bunge hilo, litakutana tena Jumanne ya tarehe 31 Agosti 2021, jijini Dodoma.
Majaliwa amesema, Serikali inachukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na COVID-19 “hatua hizo ni pamoja na kutoa miongozo zaidi ya 15 ya namna bora ya kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo.”
“Serikali imeimarisha ukaguzi wa wasafiri wote wanaoingia nchini kwa kuongeza wataalamu wa afya katika maeneo yote ya mipakani.”
Majaliwa amesema “kufunga vifaa vya kisasa vya kupima dalili za awali za ugonjwa huo, kuimarisha huduma za upimaji katika maeneo mbalimbali nchini na kuweka mfumo wa kielektroniki wa kupokea majibu ya vipimo ndani ya saa 24 baada ya kupima.”
Amesmea, tayari Serikali inafanyia kazi mapendekezo ya kamati ya wataalamu iliyoundwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan “na tutaendelea kuwajulisha waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla hatua za utekelezaji wake.”
Majaliwa amebainisha mambo saba ambayo wananchi wanapaswa kuyazingatia ni pamoja na;
Mosi: Kuendeleza tabia ya kunawa mikono mara kwa mara kwa maji tiririka na sabuni katika maeneo yote yenye mikusanyiko ikiwemo katika nyumba za ibada, masoko, vituo vya mabasi na daladala, vyuo na shule na kwenye sherehe mbalimbali. Aidha, tunapokosa maji tiririka na sabuni, tutumie vitakasa mikono (sanitizer);
Pili: Uvaaji wa barakoa safi na salama, ambayo umetengeneza mwenyewe au umenunua kwa watengenezaji waliothibitishwa hapa nchini. Katika hili, nisisitize kwa wataalamu wa afya kutoa elimu juu ya uvaaji sahihi wa barakoa sambamba na kuhimiza matumizi ya barakoa kwenye maeneo yote yenye msongamano wa watu;
Tatu: Kuepuka misongamano isiyo ya lazima ikiwemo kwenye vyombo vya usafiri, kwenye misiba, nyumba za ibada, kwenye mipira na hivyo kuzingatia kukaa umbali wa mita moja au zaidi kutoka mtu mmoja hadi mwingine na kuhakikisha maeneo hayo yanakuwa na mzunguko wa hewa wa kutosha;
Nne: Kujenga tabia ya kufanya mazoezi mara kwa mara, kulingana na hali ya afya ya mtu, na mazingira aliyonayo kama vile, kutembea kwa kasi kwa muda usiopungua dakika 30 au zaidi, hadi kutoka jasho, kuruka kamba, kukimbia mwendo unaoona unakufaa;
Tano: Kuzingatia lishe bora inayojumuisha matunda na mboga za majani kulingana na mazingira ya vyakula vya asili katika eneo analoishi mtu. Pia, kutumia bidhaa za tiba asili kama inavyoelimishwa na Wizara ya Afya kupitia Baraza la Tiba Asili;
Sita: Kwa wale wenye umri mkubwa, wenye uzito uliopitiliza na wenye magonjwa sugu kama pumu, shinikizo la juu la damu, kisukari, magonjwa ya moyo na figo wachukue hatua madhubuti zaidi za kujikinga na maambukizi; na
Saba: Kuwahi matibabu kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, mara waonapo dalili za ugonjwa wa COVID-19 kama mafua makali, maumivu ya koo, maumivu ya kichwa, uchovu wa mwili, kupumua kwa shida, kukosa hamu ya kula na kupoteza uwezo wa kunusa harufu mbalimbali.
Leave a comment