WAFANYABIASHARA wadogo maarufu kama ‘wamachinga’ wameiomba Serikali kupitia upya uamuzi wake wa kutaka kuwaondoa katika maeneo ya pembezoni mwa barabara katika soko la Kariakoo kwani ni maeneo ambayo wameyazoea na yana uhakika wa wateja. Anaripoti Helena Mkonyi na Mwanaharusi Abdallah TUDARCo … (endelea).
Wamachinga hao wametoa kauli hiyo leo tarehe 10 Septemba 2021 siku moja baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, kuagiza uongozi wa jiji la Ilala kuwa ifikapo Jumatatu uje na suluhisho kuhusu wafanyabiashara hao wanaoziba njia za watembea kwa miguu.
Mkuu huyo wa mkoa alisema ‘‘Serikali inawapenda lakini tuheshimu sheria kwa ajili yetu tusije tukaminya haki za watu wengine… Jumatatu wanakaa watakuja na mpango ambao utatupa muelekeo wetu njia hizi zote zibaki wazi.’’
Aidha, wakizungumza na Mwanahalisi Online wamachinga hao wameeleza kushangazwa na uamuzi wa serikali ya sasa kutofauti na uamuzi wa Serikali ya awamu ya nne ambayo iliwaruhusu wamachinga hao bila kuwabughudhi.
“Hapo awali tuklikuwa tukinyang’anywa kwa nguvu vitu vyetu na wakati mwingine biashara zetu kuharibiwa, sasa naona tunaelekea kulekule. Alisema Amina Hassan mmoja wa wafanyabiashara hao katika eneo la Msimbazi Kariakoo.
Hoja hiyo iliungwa mkono na mfanyabiashara mwingine aliyejitambulisha kwa jina la Adam kwamba Serikali sasa inawachanganya.
“Katika utawala uliopita wa aliyekuwa rais wa awamu ya tano hayati Dk. John Magufuli aliruhusu kufanya biashara katika maeneo hayo lakini sasa tunahamishwa,” amesema.
Leave a comment