BAADA ya kukubali kipigo cha mabao 2 – 0, dhidi ya Zambia kwenye michuano ya kombe la Mataifa Afrika, Timu ya Taifa ya Tanzania imeweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kufungwa mabao mawili toka kuanza kwa michuano hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Michuano hiyo ambayo ilianza siku ya Jumamosi tarehe 16 Januari 2021 mpaka sasa imepigwa jumla ya michezo saba, huku kukiwa hakuna timu iliyopoteza kwa mabao mawili.
Siku ya ufunguzi ilipigwa michezo miwili ambapo wenyeji Cameroon waliibuka na ushindi wa bao 1-0, mbele ya Zimbabwe, huku mchezo wa pili uliwakutanisha Mali ambao waliibuka na ushindi wa bao1-0, dhidi ya Burkina Faso.
Michezo mingine iliwakutanisha Libya ambao walikwenda sare ya bila kufungana dhidi ya Niger, huku Morocco wakifanikiwa kuwalaza Togo kwa bao 1-0.
Congo walikubali kichapo cha bao 1-0, kutoka kwa ndugu zao Congo Dr, na mchezo mwengine uliwakutanisha Rwanda dhidi ya Uganda ambao walitoka suluhu ya bila kufungana.
Stars ambayo ilicheza mchezo wake wa kwanza wa kundi D na kupoteza pointi tatu ambazo zingeweza kuwaweka vizuri kwenye msimamo.
Mabao ya Zambia kwenye mchezo huo yalifungwa na Colkins Sikombe kwa njia ya mkwaju wa penalti mara baada ya mlinzi wa Taifa Stars, Shomary Kapombe kunawa mpira kwenye eneo la hatari.
Bao la pili la Zambia likapachikwa wavuni na Emmanuel Chabula na kukamilisha idadi ya mabao hayo kwenye mchezo huo.
Kwa mantiki hiyo Stars imebakiksha michezo miwili dhidi ya Guimea na Mali ili kujua hatma yao kufuzu katika raundi inayofuata.
Michuano hiyo inafanyika nchini Cameroon na ilifunguliwa na Rais wa Shirikisho la Mpira Duniani (FIFA), Gianni Infantino ambaye alishuhudia mchezo wa ufunguzi kati ya wenyeji Cameroon dhidi ya Zimbabwe.
Leave a comment