KIONGOZI wa kiroho wa Kanisa Katoliki la All Saints Cathedral, Nairobi nchini Kenya, Sammy Wainaina amemshangaa Rais wa nchi hiyo, Uhuru Kenyatta kwa ‘kulialia’ kwamba Serikali yake imeelemewa na ufisadi. Inaripoti BBC …(endelea).
Amesema, kama Rais Kenyatta analialia kwa kupoteza mamilioni ya fedha kila mwezi, nani anapaswa kumaliza tatizo hilo wakati ana kila kitu cha kukabiliana na hali hiyo?
“Unawaambia nini Wakenya unapokiri hilo? Kwamba umeshindwa? Ni nani sasa atakayeinusuru Kenya kama Rais hawezi kutunusuru?” amehoji
“Rais, una tume ya maadili na kupambana na rushwa, una mkurugenzi wa mashitaka ya umma, una huduma za ujasusi, una kila uwezo wa serikali wa kukabiliana na ufisadi. Serikali inafahamu yule anayeiba pesa za Wakenya, au serikali inahusika katika kuiba?”
Wainaina alitoa kauli hiyo kwenye mahubiri yake Jumapili ya wiki iliyopita, video yake imetembea kwa kasi kubwa kwenye mitandao ya kijamii huku Wakenya wakitoa maoni mbalimbali hasa ya kumpongeza kwa kile walichoita, kusema ukweli.
Pia, Wainaina alikosoa kampeni inayoendelea kuhusu Katiba nchini Kenya ambayo itawezesha nyadhifa za waziri mkuu na naibu wake kubuniwa katika serikali.
“Tunapesa kwa ajili ya maridhiano ya kitaifa (BBI), ambayo itawanufaisha watu wachache tu walioko katika nafasi za juu za uongozi, lakini hatuna pesa za kujenga shule, halafu watoto wetu wanalazimishwa kusomea chini ya miti,” alisema.
Akikebehi Wakenya ‘wanaoshabikia’ ukabila amesema “ngoja niwakumbshe Wakenya kwamba, wakati mtu wa kabila lako anakuwa rais au anachukua viti vitano vya juu vya uongozi, utabakia kuwa masikini.”
Leave a comment